TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI 29/08/2016 MAAZIMIO YA KIKAO CHA BARAZA KUU LA UONGOZI LA TAIFA KATIKA KIKAO CHAKE CHA DHARURA KILI...
TAARIFA KWA VYOMBO VYA
HABARI
MAAZIMIO YA KIKAO CHA
BARAZA KUU LA UONGOZI LA TAIFA KATIKA KIKAO CHAKE CHA DHARURA KILICHOFANYIKA
JANA, JUMAPILI YA TAREHE 28/08/2016 KATIKA UKUMBI WA MAKAO MAKUU YA CHAMA,
OFISI ZA VUGA.
Ndugu Waandishi wa habari,
Awali ya yote naomba
nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uhai na uzima wa afya na
tukaweza kukutana hapa asubuhi hii ya leo. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu pia kwa
kuijaalia nchi yetu kuendelea kubaki katika hali ya amani na utulivu licha ya
matatizo mengi yanayotukabili.
Pili, nichukue fursa hii
kukushukuruni nyinyi waandishi wa habari kwa kuitikia wito wetu na kuja
kutusikiliza. Ni imani yangu kuwa kama ambavyo mmekuwa mkitupa mashirikiano
mazuri katika kuwafikishia wananchi yale ambayo chama chetu kupitia kwenu
kimekuwa kikiyatolea taarifa, kwa uzito wa kipekee taarifa hii nayo
mtawafikishia Watanzania wote kupitia vyombo vyenu vya habari.
Ndugu Waandishi wa habari,
Tumewaita leo hii
kuwaeleza juu ya maazimio ya kikao cha Baraza Kuu la Uongozi la Taifa katika
kikao chake cha dharua kilichofanyika jana, Jumapili ya tarehe 28/08/2016
Katika ukumbi wa Makao Makuu ya Chama, ofisi za Vuga. Kikao hicho
kilichoongozwa na Mwenyekiti wa muda Mhe, Hamidu Hassan Bobali, Mbunge wa Jimbo
la Mchinga kilihudhuriwa wa Wajumbe 46 katika ya Wajumbe 60.
Ndugu Wandishi wa Habari,
Kama mnavyojua tarehe
21/08/2016 Chama Cha Wananchi – CUF kilikuwa na Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa
uliofanyika katika ukumbi wa Blue Pearl, Ubungo Plaza, Dar es Salaam. Mkutano
huo ulikuwa na agenda mbili kuu, ambazo ni:-
1. Kupokea barua ya
Profesa Ibrahim Haruna Lipumba ya kujiuzulu nafasi yake ya uenyekiti ya tarehe
05/08/2015; na
2. Kufanya Uchaguzi wa
kujaza nafasi zilizo wazi - Mwenyekiti Taifa, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe wanne
wa Baraza Kuu la Uongozi la Taifa.
Kufuatia hujuma za
makusudi zilizoandaliwa kwa mashirikiano ya maadui wa ndani na nje ya chama,
aliyekuwa Mwenyekiti wa muda wa Mkutano Mkuu Maalum, Mhe Julius Mtatiro
alilazimika kuakhirisha Mkutano ule mara baada ya kumalizika kwa ajenda ya
kwanza ambapo Mkutano Mkuu uliridhia kujiuzulu kwa Profesa Ibrahimu Haruna
Lipumba kwa azimio lililoungwa mkono na wajumbe 476 dhidi ya wajumbe 14
waliokataa. Hivyo basi agenda namba 2 haikuwahi kukamilishwa, na kwa hivyo
haikufanyiwa maamuzi.
Kikao cha Baraza Kuu la
Uongozi, kilichokaa jana kimejadili kwa kina juu ya hujuma za kuvuruga Mkutano
Mkuu Maalum wa tarehe 21/08/2016. Baraza kuu limesikitishwa sana na kitendo
kile ambacho mbali ya kukisababishia chama hasara ya zaidi ya Shillingi milioni
600, pia kimepelekea kuharibu taswira ya chama ndani na nje ya nchi.
Baraza Kuu lilipata nafasi
ya kupokea maelezo ya kina kutoka kwa wajumbe mbali mbali hasa wale wanaotokea
Tanzania Bara walioeleza kwamba hujuma zilizofanywa kuvuruga Mkutano Mkuu
Maalum wa Taifa wa tarehe 21 Agosti, 2016 hazikuwa za bahati mbaya au za
kushtukiza bali ni matokeo ya njama na mbinu ovu na chafu ambazo zimekuwa
zikipangwa na kutekelezwa chini kwa chini kwa muda mrefu. Wajumbe wa Baraza Kuu
la Uongozi la Taifa walieleza kwa ushahidi jinsi baadhi ya viongozi wa Chama
walioaminiwa na kupewa nyadhifa za juu walivyogeuka na kuanza kutumiwa na
maadui wa nje ya Chama kukihujumu Chama.
Baraza Kuu limezingatia
kuwa CUF ni chama cha kistaarabu, ni Chama cha Kidemokrasia na ni Chama chenye
kutoa matumini ya mabadiliko ya kweli kwa Watanzania walio wengi. Vurugu
zilizojitokeza ni aibu na fedheha kwa chama chetu mbele ya macho ya Watanzania
na wapenda demokrasia.
Baraza Kuu la Uongozi la
Taifa limeridhika kwamba watu hao waliokuwa vinara wa vurugu na njama hizo ovu
walipewa nafasi mara kadhaa kujirekebisha dhidi ya mwendo wao huo dhidi ya
Chama lakini waliendelea na vurugu na hujuma zao hizo. Kwa hatua iliyofikia,
Baraza Kuu limeona halina njia nyengine ya kukinusuru Chama isipokuwa kuchukua
hatua kali na madhubuti kukilinda Chama ambao ni wajibu wake kikatiba.
Kwa msingi huu basi,
Baraza Kuu la Uongozi la Taifa kwa kauli moja (unanimously) limeamua kuchukua
hatua za kinidhamu kwa viongozi na wanachama mbali mbali waliohusika kwa njia
moja au nyengine katika kuchochea vurugu zile. Baraza kuu limechukua hatua
mbili kubwa ambazo ni kutoa karipio kali, kusimamisha na kufukuza uanachama
wahusika wote walioshiriki kuchochea vurugu hizo.
Viongozi waliopewa karipio
kali kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(b) ambao ni wajumbe wa
Baraza Kuu la Uongozi la Taifa ni:
1. Rukiya Kassim Ahmed na
2. Athumani Henku
Viongozi waliosimamishwa
uanachama kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(c), hadi hapo
watakapopata fursa ya kujieleza mbele ya Baraza Kuu ni;
1. Prof Ibrahim Haruna
Lipumba
2. Magdalena Sakaya
3. Abdul Kambaya
4. Ashura Mustafa
5. Omar Mhina Masoud
6. Thomas Malima
7. Kapasha M. Kapasha
8. Maftaha Nachumu
9.Mohamed Habib Mnyaa
10. Haroub Shamis
na
na
11. Mussa Haji Kombo
Mwanachama aliyefukuzwa
chama ambaye alipata fursa ya kujieleza mbele ya Baraza Kuu na kikao kuamua
kumfukuza chama kwa mujibu wa Katiba ya Chama, Ibara ya 83 (5)(c) ni aliyekuwa
Kaimu Katibu Mtendaji wa Jumuiya ya Wazee wa CUF (JUWACUF), Shashu Lugeye.
Kufuatia maamuzi hayo,
Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limewateua viongozi mbali mbali kukaimu nafasi
mbali mbali zilizoachwa wazi.
Kwa kuzingatia kwamba
kutokamilika kwa Mkutano Mkuu Maalum wa Taifa wa tarehe 21 Agosti, 2016
kulipelekea kushindwa kufanyika kwa uchaguzi wa Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti
wa Chama, Baraza Kuu la Uongozi la Taifa limetumia uwezo liliopewa na Katiba ya
Chama, Ibara ya 101 na 118, kuunda Kamati ya Uongozi ambayo itakuwa ikifanya
kazi za Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti hadi hapo uchaguzi wa kujaza nafasi
hizo utakapofanyika. Baraza Kuu la Uongozi limewateua wafuatao kuwa wajumbe wa
Kamati hiyo ya Uongozi:
1. Mhe. Julius Mtatiro –
Mwenyekiti;
2. Mhe. Katani Ahmed
Katani – Mjumbe; na
3. Mhe. Severina Mwijage –
Mjumbe.
Aidha Baraza Kuu la
Uongozi la Taifa, kwa kufuata Ibara ya 105 (1) na (3) ya Katiba ya Chama,
limemteua Mhe. Joran Bashange kuwa Kaimu Naibu Katibu Mkuu wa Chama kwa upande
wa Tanzania Bara na Mhe. Mbarala Maharagande kuwa Kaimu Naibu Mkurugenzi wa
Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma hadi hapo nafasi hizo zitakapojazwa
rasmi kwa mujibu wa masharti ya Katiba ya Chama.
Mwisho, Baraza Kuu la
Uongozi la Taifa linawahakikishia wanachama na wapenzi wake na Watanzania wote
kwa ujumla kuwa Chama Cha Wananchi – CUF kipo imara na makini na katu
hakitoyumbishwa kwa hila na njama ovu na chafu zinazofanywa na maadui wa chama
hichi. Tangu kuasisiwa kwake, CUF imeandamwa na maadui wa kila aina, na
imepitia katika misuko suko mingi. Tunaamini hila na njama hizo ovu zimekuwa zikielekezwa
CUF kwa kutambua kwamba Chama hichi ndicho kinachobeba dhamira ya dhati ya
kuleta mabadiliko ya kweli hapa nchini.
Kutokana na umadhubuti,
umakini na uimara wa Katiba ya Chama na safu ya viongozi wake, CUF imeweza
kuvuka salama kila ilipoingia katika misuko suko hiyo na kwa hivyo, hata wimbi
hili lililoonekana kukitikisa Chama limekabiliwa ipasavyo na sasa kazi iliyopo
mbele yetu ni kuendeleza harakati za kisiasa za kuwaletea Watanzania wa Bara na
Zanzibar mabadiliko wanayoyataka.
HAKI SAWA KWA WOTE
Nassor Ahmed Mazrui
NAIBU KATIBU MKUU CUF
COMMENTS