Baadhi ya waliohudhuria kwenye kilele cha Maadhimisho ya miaka 55 ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam wakimsikiliza Waziri Mkuu, Kassim ...
HOTUBA
YA WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA MHESHIMIWA KASSIM MAJALIWA
(MB) ILIYOTOLEWA KATIKA SHEREHE ZA KILELE CHA MAADHIMISHO YA MIAKA 55 TANGU
KUANZISHWA KWA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM ILIZOFANYIKA KATIKA UKUMBI WA
NKRUMAH TAREHE 25 OKTOBA, 2016
Mheshimiwa
Prof. Joyce Ndalichako (MB), Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia;
Mheshimiwa
Peter Ngumbullu, Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;
Mheshimiwa
Jaji Joseph Sinde Warioba, Rais wa Jumuiya ya Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es
Salaam na Makamu wa Mwenyekiti wa Baraza la Chuo;
Prof. Rwekaza
Mukandala, Makamu Mkuu wa Chuo;
Wajumbe wa Baraza la Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam;
Manaibu wa Makamu Mkuu wa
Chuo: Prof. Florens Luoga, Prof. David Mfinanga na Prof. Kimambo;
Viongozi
Waandamizi wa Serikali waliopo;
Waheshimiwa
Wabunge waliopo hapa;
Waheshimiwa
Mabalozi wa Nchi za Kigeni;
Wawakilishi
wa Mashirika ya Kimataifa;
Wanataaluma
na Wafanyakazi wengine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam;
Wanafunzi
na Wanajumuiya wote wa Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam;
Wageni
Waalikwa;
Mabibi
na Mabwana.
SHUKURANI
- Napenda kutumia fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuwa hapa siku ya leo kusherekea maadhimisho haya ya Miaka 55 ya kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
- Pili, ninawashukuru waandaji wa tukio hili kwa heshima kubwa mliyonipa kuwa mgeni rasmi katika tukio hili muhimu na la kihistoria. Kwangu mimi ni jambo la fahari, furaha na heshima kubwa kupata fursa ya kushiriki pamoja nanyi katika shughuli hii adhimu.
- Kuna sababu nyingi zinazonifanya kufurahia fursa hii ya kushiriki katika maadhimisho haya. Kwanza kabisa, kama mnavyofahamu, mimi ni mdau wa elimu. Mimi ni mwalimu ambaye ninayeitumikia sekta hii kwa muda wa kutosha. Pili, kama Kiongozi Mwandamizi wa Serikali iliyopo madarakani hivi sasa, nina dhamana ya kushirikiana na wananchi wenzangu katika kuendeleza na kuboresha utoaji elimu kwa jamii yetu, jukumu ambalo pia ni kiini cha wajibu na utendaji wa Chuo hiki. Tatu, mimi ni mhitimu wa Chuo hiki. Chuo hiki kimenilea na kunipatia ujasiri na maarifa; ambayo yamekuwa nyenzo muhimu katika utendaji wangu wa kazi kwa miaka mingi.
- Hivyo, ninatoa shukrani zangu za dhati kwa kupata fursa hii. Ninaushukuru uongozi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa kubuni na kuandaa maadhimisho haya ya kihistoria. Niseme tu kwa uwazi kwamba, kushiriki kwangu katika sherehe hii kunanipa fursa adimu ya kurudi kwa mama ili kuungana na wahitimu wenzangu, wa miaka ya nyuma na wa hivi karibuni, pamoja na wadau wote wa Chuo chetu hiki, katika kutambua upya jukumu kubwa lililotekelezwa na chuo hiki katika maendeleo ya nchi yetu.
HISTORIA YA CHUO KIKUU CHA
DAR ES SALAAM
Kuanzishwa
Kwa Chuo
Mheshimiwa
Mwenyekiti,
Ni vyema tukajikumbusha
kwamba Chuo hiki kilianza kikiwa kidogo sana, na kwamba kuanzishwa kwake
kulihitaji ushupavu na moyo wa kizalendo. Ni muhimu kuyakumbuka na kuyaelezea
mambo haya kwa ufasaha, kwani si wengi wanaofahamu nafasi ya Chuo hiki katika
historia ya nchi yetu. Kwa bahati nzuri, baadhi ya mambo haya yamehifadhiwa
katika kumbukumbu za kihistoria. Wakati wa sherehe za uzinduzi wa Chuo hiki
hapo mwaka 1961, aliyekuwa wakati ule Waziri Mkuu wa Tanganyika, Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere, alisema, na hapa namnukuu:
“Chuo hiki
kimeanzishwa kwa dharura. Mapendekezo yote ya kuanzisha Chuo Kikuu Kishirika
nchini Tanganyika yalitaja tarehe ya baadaye sana ya kuanzishwa huko. Lakini
Serikali yangu iliona kwamba suala hili lina umuhimu wa juu kabisa kielimu.
Baadhi ya watu wamesema kuwa ule ilikuwa uamuzi wa kisiasa. Kweli, ulikuwa ni
uamuzi wa kisiasa”. Mwisho wa
kunukuu.
Ni dhahiri kwamba kuanzishwa
kwa Chuo hiki kulitokana na ndoto sahihi ya viongozi waasisi wa nchi yetu,
ndoto ambayo ilikataa dhana ya kuwa na nchi huru isiyokuwa na mpango thabiti wa
kuwapa wananchi wake elimu ya juu. Badala yake, waasisi wa taifa hili
walichukua hatua sahihi ya kuanzisha taasisi ya elimu ya juu itakayokuwa
chemchemi ya maarifa na mahali pa kuwatayarishia wataalamu wa ngazi za juu
watakaochochea maendeleo. Kwa kupigania na kufanikiwa kuanzisha Chuo hiki,
waasisi wa Taifa letu walidhihirisha uwezo wao wa kuona mbali na uzalendo wa
hali ya juu. Viongozi hao walikuwa werevu, na walielewa vizuri kwamba msingi wa
maisha na maendeleo ya jamii yoyote iwayo ile ni elimu, na kwamba uwekezaji
katika elimu ni jambo lisilokwepeka kwa Serikali inayotaka kuwakwamua watu wake
kutoka katika adha ya umaskini, ujinga na maradhi.
Waasisi wa
Chuo
Ndugu Wanajumuiya ya Chuo na
Wageni Waalikwa,
Ni vyema basi,
tunaposherehekea miaka 55 ya Chuo hiki, tufanye huku tukiwakumbuka na
kuwashukuru viongozi waasisi wa nchi yetu na wote walioshiriki katika
kukianzisha na kukiendeleza Chuo hiki hadi hapa kilipofikia. Kwa mantiki hiyo,
sherehe hizi, ambazo zilianza rasmi jana, vilevile ni sherehe za kuwapongeza na
kuwatambua watu wote waliofanya uamuzi makini wa kuanzisha Chuo Kikuu hata
kabla nchi yetu haijapata uhuru kamili. Tunawapongeza na kuwashukuru wote
walioshiriki katika kutekeleza jukumu lile hasa kwa sababu hawakutishika na
changamoto za kuanzisha taasisi kama hii katika nchi ambayo ilikuwa ikikabiliwa
na changamoto za umaskini, maradhi na ujinga.
Mheshimiwa Mwenyekiti,
Siyo rahisi kuwakumbuka wote
waliohusika katika kutekeleza jukumu lile la kihistoria, lakini hatuwezi
kusahau mchango wa Waziri Mkuu wa siku zile, Mwalimu Nyerere, pamoja na Baraza
lake la Mawaziri. Vile vile, si rahisi kusahau michango maalum iliyotolewa na
Profesa Cranford Pratt, aliyekuwa Rasi (Principal) wa kwanza wa Chuo, na pia
Profesa Arthur Brian Weston, ambaye alikuwa Mkuu wa kwanza wa Kitivo cha Kwanza
kuanzishwa Chuoni, yaani Kitivo cha Sheria, pamoja na wanafunzi wake 12
waanzilishi, ambao baadhi yao naambiwa waliweza kuhudhuria sherehe za miaka 50
ya Chuo zilizofanyika mwaka 2011 katika ukumbi huu. Tuwakumbuke pia wanataaluma
wote waanzilishi pamoja na viongozi waendeshaji wa Chuo ambao walifanya kazi
kubwa ya kuweka msingi imara kwa ajili ya maendeleo ya taasisi hii.
Chuo Kikuu
Cha Umma
Ndugu Wanajumuiya na Wageni
Waalikwa,
Kwa kuwa Chuo hiki
kilianzishwa katika miaka ya awali ya uhuru wa nchi yetu, hakijawahi kuendekeza
sana kasumba za kikoloni kama ilivyokuwa katika baadhi ya vyuo vikuu vya
Kiafrika vilivyoanzishwa katika miaka ya 1950 na 1960. Tangu awali Chuo hiki
kimechukua taswira ya kuwa Chuo cha Umma, kwa Kiingereza People’s
University. Inatia moyo kufahamu kwamba dhana hiyo ya People’s
University imeendelea kutekelezwa hadi hivi sasa. Nimefarijika kufahamu
kwamba uongozi wa Chuo umekuwa ukifanya jitihada za makusudi kuhakisha kuwa
taaluma zinazotolewa hapa zinaendelea kuwa chimbuko la maarifa yanayohitajika
katika kuboresha maisha ya wananchi na kuleta maendeleo ya nchi kwa ujumla.
Matumaini yangu ni kwamba jitihada hizi zitaendelea na Chuo kitaendelea kudhihirisha
kwa vitendo kuwa kiko karibu na wananchi wa kawaida.
UMUHIMU WA MAADHIMISHO YA
MIAKA 55 YA CHUO KIKUU CHA DAR ES SALAAM
Mabibi na Mabwana,
Leo ni siku ambayo
tunahitimisha Maadhimisho ya Miaka 55 tangu kuanzishwa kwa Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam. Sherehe kama hizi hutoa fursa kwa wahusika kutathmini mafanikio
waliyopata na changamoto walizopambana nazo katika kipindi kilichopita. Ni
fursa pia ya kufikiria maendeleo ya taasisi husika kwa siku zijazo. Ukweli huo
huonekana katika kila aina ya jubilei, lakini pale tunaposherehekea miaka 55 ya
taasisi kama Chuo Kikuu cha Dar es Salaam umuhimu wa kufanya mambo haya unakuwa
mkubwa zaidi. Kwa hiyo, sote tutambue kwamba ni wajibu wa kila mmoja wetu
kuchangia kikamilifu zoezi la kutathmini mafanikio ya Chuo hiki kikongwe,
changamoto ambazo Chuo kimekumbana nazo na kusaidia kuchangia jitihada za
kukiendeleza zaidi Chuo hadi kufikia mafanikio makubwa.
CHANGAMOTO NA MIKAKATI
Mabibi na Mabwana,
Maslahi ya watumishi,
wanataaluma na waendeshaji:
Ninafahamu kuwa yapo madai
mbalimbali ikiwemo malimbikizo ya mishaara kwa watumishi hususan baada ya
kuanza kwa muundo wa pamoja wa wanataaluma wa vyuo vikuu vya umma. Serikali ya
awamu ya tano imedhamiria kuhakikisha inaondoa malimbikizo ya madai kwa
watumishi wote wa umma. Mojawapo ya mikakati ya kukamilisha azma hii ni pamoja
na; kufanya uhakiki wa taarifa za kiutumishi kwa watumishi wa umma ili kubaini
watumishi hewa; zoezi ambalo limesaidia kuwabaini watumishi wa umma hewa
wapatao 16,500 kufikia tarehe 20/10/2016. Baada ya zoezi hilo tutarudia
uhakiki wa madeni yote yaliyowasilishwa Serikalini na kasha tutalipa madeni ya
watumishi wote. Natumaini kuwa wote mnakumbuka, Mheshimiwa Rais alitoa
tamko la kupunguza kodi kwenye mshahara kuanzia Julai 2016. Aidha, Serikali
inaendelea na maboresho na kuimarisha maslahi kwa watumishi wote wa umma
kupitia bodi ya mishahara na motisha mara tutakapokamilisha tutapanga upya
mishahara na motisha kwa watumishi.
Wahadhiri Waandamizi na
Maprofesa katika Vyuo vya Umma
Mabibi na Mabwana,
Ninatambua kuwa katika vyuo
vya umma kuna upungufu mkubwa wa wahadhiri waandamizi na maprofesa na hivyo
kuathiri hali ya utoaji wa taaluma kwa fani za “Post –Graduates”. Ninajua kuwa
pamoja na sababu nyingine, hali hii inachangiwa pia na masharti ya ajira za
mikataba kwa wahadhiri waandamizi kuwa miaka 65 na maprofesa kuwa miaka 70.
Serikali itaendelea kuweka kipaumbele cha upatikanaji wa fedha za kutosha kwa
ajili ya mafunzo. Wakati huohuo vyuo vya elimu viweke taratibu na mipango
endelevu ya kurithishana (kuachiana nafasi) “Succession Plan”. Jambo hii ni
muhimu sana kwani bila hivyo, wakati wote kutakuwa na “Gap” kubwa katika utoaji
wa taaluma. Aidha, Serikali itatoa ushirikiano wa kutosha katika utekelezaji wa
mipango hii ya kuwa na watalaamu wa kutosha katika vyuo. Kwa upande mwingine
Serikali itaendelea kutekeleza majukumu ya kuwaajiri wanataaluma na wafanyakazi
wapya pale wanapohitajika.
Hali ya
upatikanaji wa fedha za uendeshaji
Mabibi na
Mabwana,
Kwa wakati tofauti nimekuwa
napata malalamiko juu ya vyuo kutopata fedha za kutosha za uendeshaji (OC) na
hivyo kuathiri utoaji wa taaluma. Serikali hii imeamua kuimarisha ukusanyaji wa
mapato ya ndani ili iweza kumudu mjukumu ya uendeshaji wa Serikali bila ya
kutegemea kwa kiwango kikubwa wafadhili wa nje. Matarajio yetu ni kuwa kutokana
na kuongezeka kwa makusanyo na kukua kwa uchumi, Serikali itaimarisha hali ya
upatikanaji wa fedha za uendeshaji na maendeleo katika taasisi zote za umma.
Aidha, vyuo viimarishe ubunifu, umakini na uhalisia ili kukuza makusanyo ya
ndani na kuhakikisha matumizi yanafanyika kwa kuzingatia tija (value for
money).
Mikopo
ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu
Mabibi
na Mabwana,
Serikali
kupitia Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania ametoa ufafanuzi wa namna ya ya kutekeleza utoaji mikopo na Wizara
ya Elimu, Sayansi na Teknolojia inaendelea kufanya uhakiki wa taarifa za
waombaji wa mikopo. Ninapenda kutoa wito kwa wanufaika na waombaji wote wa
mikopo wahakikishe kuwa wanatoa taarifa zilizo sahihi na za uhakika. Hata
hivyo, Serikali ilishaongeza bajeti ya mikopo ya Elimu ya Juu kutoka Shilingi
Bilioni 340 mwaka 2015/2016 hadi Bilioni 483 kwa mwaka 2016/2017.
Matokeo
ya Kukua kwa Sekta ya Elimu
Mabibi
na Mabwana,
Kutokana
na kukua kwa sekta ya elimu hususan ushiriki wa sekta binafsi katika sekta ya
elimu kumekuwepo na changamoto kubwa ya vyuo kadhaa nchini kuanzisha programu
za masomo ambazo haziendani na mahitaji halisi ya taifa letu pamoja na soko la
ajira. Ninaamini kuwa jumuiya ya wanataaluma na viongozi wa Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam mnaelewa wajibu na majukumu yenu katika kutekeleza azma ya kukipeleka
Chuo mbele kutoka hapa kilipo. Nimeelezwa mambo mengi yanayofanyika ili
kuboresha mfumo wa Chuo na kuongeza ufanisi katika utoaji maarifa, ikiwa ni
pamoja na kuanzisha programu mpya za masomo kulingana na mahitaji ya taifa letu
kwa hivi sasa. Napenda kusisitiza Tume ya Vyuo Vikuu Nchini kuhakikisha kuwa
program za masomo zinazoanzishwa na vyuo vikuu zinazingatia mahitaji ya Taifa
na soko la ajira.
Mabibi
na Mabwana,
Serikali
kwa upande wake itaendelea kutekeleza majukumu yake ya kawaida, ambayo ni
pamoja na kuendelea kuwaajiri wanataaluma na wafanyakazi wapya pale
wanapohitajika; kuwapa stahili zao wale wanaostaafu; kutoa mikopo kwa wanafunzi
kulingana na sera iliyokubalika; na kulipa gharama za uendeshaji wa Chuo kadiri
ya taratibu za kibajeti. Licha ya hayo, Serikali pia itachukua hatua madhubuti
kushughulikia changamoto zinazokwamisha utendaji na ustawi wa Chuo.
Hali ya
Miundombinu ya Chuo
Mabibi na Mabwana,
Natambua
kutokana na ukubwa na umri wa Chuo ziko changamoto kadhaa zinazohusu mazingira
ya kujifunzia na kufundishia hususan utoshelevu wa miundombinu kama vyumba vya
mihadhara, maabara, mabweni, ofisi na vifaa mbalimbali. Napenda kuwahakikishia
wanajumuiya ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kuwa Serikali itaendelea kulifanyia
kazi tatizo la uhaba wa mabweni ya wanafunzi, na itachukua hatua kushughulikia
pia tatizo la upungufu wa maabara, vifaa vya kufundishia na ofisi za
wafanyakazi. Tutayatekeleza haya kwa kuzingatia umuhimu wa miradi husika katika
uendeshaji na maendeleo ya Chuo pamoja na uwezo wa Serikali kifedha. Mheshimiwa
Rais amekwishaonesha mfano wa hatua ambazo Serikali ya Awamu ya Tano itakuwa
inachukua katika kushughulikia kero sugu zinazokabili Chuo hiki. Sote
tumefurahishwa na kasi ya utekelezaji wa mradi unaoendelea hapa chuoni wa
ujenzi wa mabweni ya wanafunzi, ambao utawapa wanafunzi takribani 3,840 nafasi
za malazi chuoni badala ya kupanga mitaani. Aidha, Serikali imeshaanza kutenga
fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya taasisi za elimu ya juu na
nyinginezo. Tumefanya hivyo katika bajeti ya mwaka huu wa fedha, na tutaendelea
kufanya hivyo katika bajeti zijazo. Lengo ni kuziwezesha taasisi hizo, Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam kikiwepo, kufanyia ukarabati unaostahiki miundombinu
yao iliyochakaa. Kwa kutumia fedha hizo, taasisi za umma zitaweza pia,
kutekeleza miradi midogo midogo ya maendeleo.
HITIMISHO
Mabibi
na Mabwana,
Matumaini
yangu ni kwamba Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitaendelea kutumia changamoto
zinazojitokeza mara kwa mara kama chemchemi ya ubunifu wa mambo mapya na
mikakati yenye tija. Vilevile ninatumaini kuwa Chuo kitaendelea kuboresha uwezo
wake wa ndani wa kupata rasilimali muhimu na kuboresha utendaji wake na
kuongeza uwezo wa kujiletea maendeleo. Aidha, Serikali inategemea kuwa Chuo
hiki kitaendeleza sifa yake ya kuwa kinara katika utoaji wa taaluma kwa viwango
vya kimataifa na hivyo kuwa mfano wa ubora katika sekta ya elimu ya juu hapa
nchini na katika ukanda huu wa Afrika. Sina shaka kuwa haya yote yanawezekana
kwa kuwa yako katika uwezo wenu wa kitaasisi. Ninawahakikishia kuwa Serikali
itakuwa nanyi daima katika jitihada za kufikia ndoto yenu kuelekea mwaka 2061.
Mabibi
na Mabwana,
Ningependa
kumalizia hotuba yangu kwa kuwashukuru tena wote waliohusika katika kuandaa
maadhimisho haya na kutekeleza majukumu mbalimbali. Nawashukuru pia nyote
mliohudhuria hafla hii ambayo ndiyo kilele cha maadhimisho ya miaka 55 ya Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam.
Na sasa,
kwa mamlaka mliyonipa kama Mgeni Rasmi katika hafla hii, ninayo furaha, kutamka
kuwa Sherehe za Maadhimisho ya Miaka 55 ya Chuo Kikuu cha Dar es Slaam
zimefungwa rasmi.
Nawatakia
heri na fanaka katika shughuli zenu zitakazoendelea baada ya maadhimisho haya.
ASANTENI
SANA KWA KUNISIKILIZA
COMMENTS