MUHTASARI WA KONGAMANO LA MABADILIKO YA UENDESHAJI WA KLABU ZA SOKA TANZANIA Kongamano la mabadiliko ya uendeshaji wa klabu za soka l...
MUHTASARI WA
KONGAMANO LA MABADILIKO YA UENDESHAJI WA KLABU ZA SOKA TANZANIA
Kongamano la
mabadiliko ya uendeshaji wa klabu za soka limefanyika Jumamosi Oktoba 22, 2016
kwenye ukumbi wa Uwanja Mkuu wa Taifa, Dar es Salaam.
Kongamano hilo
lililoandaliwa na chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzani (TASWA)
lilishirikisha wadau zaidi ya 60 nchini.
Kituo cha
televisheni cha Azam kilionesha live (mubashara) kongamano hilo huku wajumbe
wakikubaliana masuala kumi ya msingi.
Kwanza wajumbe
walikubali kuwa kuna umuhimu wa kufanya mabadiliko sasa kwa sababu muundo
unaotumika kuendesha klabu za soka una matatizo mengi.
Pili iliamuliwa
klabu zijiandae vya kutosha kukaribisha mabadiliko hayo ikiwa ni pamoja na
kuboresha utawala bora (governance) kwenye uendeshaji wa klabu.
Tatu mifumo yetu
kama nchi inawezesha klabu kuwa na aina nyingi za mifumo ya kiuendeshaji hivyo
wanachama waelimishwe kwa kina kuhusu mifumo hiyo ili wachague ulio bora zaidi
kwa manufaa ya klabu zao.
Nne ili
mabadiliko haya yafanyike kwa haki, inatakiwa wamiliki wa timu hizi (wanachama)
waelimishwe vya kutosha juu ya thamani yao ili wajitambue. Kwamba
thamani ya klabu kubwa nchini haiwezi kulinganishwa na kiasi cha fedha
kinachotolewa na wawekezaji hivyo wanachama wasiingie kwenye mabadiliko wakiwa
wanyonge kwa sababu wao ndio wana mtaji mkubwa kuliko hela zinazoletwa kwa
ajili ya uwekezaji.
Tano mabadiliko
haya hayawezi kufanywa na wanachama na wawekezaji pekee bila kuishirikisha
serikali. Hivyo klabu zinapojipanga kwa mabadiliko haya zihakikishe
zinashirikisha serikali na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Sita mabadiliko
haya yasifanywe kishabiki bali yafanywe kitaalamu ili kutengeneza
msingi Imara utakaoepusha migogoro hapo baadaye.
Saba kuelekea
mabadiliko haya, hasa katika kipindi hiki ambacho uelewa wa wanachama ni mdogo,
serikali inatakiwa kulinda maslahi ya walio wengi kwa kuingilia kati pale
inapoona kuna mwelekeo wa kuwa na mabadiliko yanayominya maslahi ya walio
wengi.
Nane mpira ni
biashara ya kipekee ambayo mafanikio yake yanategemea jinsi washindani
wanavyoshirikiana. Hivyo kuelekea mabadiliko haya wanatakiwa watumike wataalamu
wa biashara ya mpira ili klabu zinapobadilika ziweke misingi itakayokubaliana
na biashara ya soka.
Tisa klabu
zinao wajibu wa kulinda hadhi zake (brand) kwa sababu eneo hilo ndio msingi wa
biashara ya mpira. Hivyo klabu zinapoelekea kwenye mabadiliko, lazima
zizingatie hadhi zao zinalindwaje.
Kumi Chama cha
Waandishi wa Habari na Michezo kiliombwa kufanya makongamao zaidi hasa
kuhusiana na aina ya mabadiliko ambayo klabu zinaweza kuingia kwa sababu
inaonekana wanachama ambao ndio wamiliki wa klabu hizi hawana uelewa wa kutosha
hivyo inawapunguzia wigo wa kuchagua aina ya mabadiliko.
SHIJA RICHARD
KATIBU WA
SEKRETARIETI
KONGAMANO LA
MABADILIKO YA UENDESHAJI WA KLABU ZA SOKA
Oktoba 24, 2016.
..................................................
TAARIFA KAMILI
UFUNGUZI
Kongamano
lilifunguliwa na Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohammed
Kiganja kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na
Michezo, Prof. Elisante Ole Gabriel.
Kiganja aliwataka
wajumbe kujadili hoja badala ya watu au timu. Alisisitiza wajumbe wajadili
mifumo na aina ya mabadiliko ambayo klabu hizi zinaweza kuelekea.
Pia aliwataka
TASWA kuhakikisha Waandishi wake wanaripoti taarifa zenye weledi na zenye
manufaa kwa familia ya wana michezo.
Aliongeza TASWA
iunde kamati ya maadili kwa ajili ya kuwawajibisha wanachama ambao wanaenda
kinyume cha maadili.
WACHANGIAJI
PROFESA PROSPER
NGOWI- Chuo Kikuu cha Mzumbe
Katika mada yake,
Profesa anasema wanachama na wadau kwa ujumla hawatakiwi kuogopa kufanya
mabadiliko au kubadilisha namna ya kuendesha vitu kwa sababu hilo ni jambo la
kawaida.
Hata hivyo
akadokeza kuwa wanachama wa Simba na Yanga hawapaswi kuwa wanyonge kuelekea
kwenye mabadiliko hayo kwa sababu mtaji wao ni mkubwa kuliko pesa zinazoletwa
na wafadhili.
"....(Wanachama)
Mtaji wao mkubwa pengine sio pesa. Mtaji wao mkubwa ni majina yaani brand ya
timu hizi. Mtaji mwingine ni historia ndefu ya timu hizi ya zaidi ya miaka 80
na ‘fan base’ kubwa sana. Pia vikombe ambazo timu hizi zimeshida ni mtaji
mkubwa sana katka meza ya majadiliano. Hii ni mitaji ambayo thamani yake ni
kubwa kuliko pesa. Kwa hiyo wenye timu hizi hawapaswi kuwa wanyonge kifedha
mbele ya wawekezaji. Thamani ya mitaji hii hasa brand ni kubwa kuliko
pesa."
Aliendelea
kueleza, "Lazima waelewe kama wanakodisha timu hizi, wanatoa na kupokea
masharti gani? Hawapaswi kupokea tuu bali nao watoe masharti. Waamue
wanawakilishwa vipi katika uendeshaji wa timu hizi katika nyanja zote? Brand ya
timu hizi zinalindwa vipi? Ni muhimu pia kujua kuwa kama mwekezaji atataka muda
mrefu wa mkataba, Lazima wenye timu wawe na muda na nafasi ya kufanya
marekebisho ktk makubaliano baada ya muda fulani, mfano miaka miwili au mitatu
badala ya kusubiri hadi mwisho wa mkataba, mfano miaka 10", anasema
Profesa Ngowi ambaye ni mtaalamu wa masuala ya uchumi na biashara.
Profesa Ngowi
anasisitiza kuwa kwa mtazamo wa kiuchumi na kibiashara mabadiliko ni jambo la
kawaida na halipaswi kuonekana la ajabu.
"Jambo hilo
linapaswa kuwa la kawaida kwa yeyote anayependa. Hakuna sababu ya kuogopa
kufanya mabadiliko au namna ya kufanya mambo" anasema Profesa Ngowi.
Anaendelea
kueleza jambo la msingi katika mabadiliko hayo ni pande zinazohusika hasa
wanachama ambao ni wamiliki wa klabu kujua ni kipi wanachokitaka.
"Inavyoonekana
wanachotaka ni hali nzuri ya kiuchumi ya timu zao. Sio jambo baya. Wawekezaji
nao wanataka maslahi ya kiuchumi nalo sio jambo baya hata kidogo," anasema
Profesa Ngowi.
PATRIC MUSUSA -
MENEJA WA MASOKO NA MIRADI KUTOKA SOKO LA HISA DSM (DSE)
Mususa
anasema klabu zinapotaka kuelekea kwenye mabadiliko hasa kwa
matarajio ya kuingia kwenye soko la hisa, kwanza zihakikishe zinabadilisha
mifumo yao iliyopo sasa ili iendane na mahitaji ya soko la hisa.
Anasema lazima
zisajiliwe kuwa kampuni na Wakala wa Usajili wa Makampuni (BRELA) na pia
ziandae taarifa za fedha.
Lazima zitatakiwa
kuwa na Bodi ya Wakurugenzi (BOD) watakaochaguliwa na wanahisa ambao ni
wanachama wamiliki wa klabu hizo.
Kila mwanahisa
atastahili kupata gawio la faida pale kampuni (klabu) yao itakapotengeneza
faida na atakuwa huru kuuza hisa yake kama anataka kuachanana na
umiliki katika klabu hiyo.
ANGETILE OSIAH,
KATIBU MKUU WA ZAMANI WA TFF
Angetile anasema
klabu zikihitaji kubadilisha mifumo yao zinatakiwa kuzingatia utawala bora kwa
kutofautisha majukumu sekretarieti na taasisi nyingine zilizopo ndani ya klabu.
Anasema ulimwengu
wa sasa mchezaji ni rasilimali(asset) inayothaminishwa kwa fedha kwenye vitabu
vya hesabu hivyo klabu lazima iwe na wataalamu watakaoweza kukabiliana na
changamoto hizo za utaalamu na nyinginezo.
Anasema klabu
lazima ziwe na kurugenzi za uendeshaji, habari, biashara, sheria, fedha na
masoko na ziajiri wataalamu kwa ajili ya kuendesha shughuli hizi. Kurugenzi
hizo zinahitaji wataalamu kama waliopo kwenye taasisi nyingine za serikali na
makampuni binafsi.
Anaongeza kuwa
uendeshaji wa klabu lazima uzingatie utawala bora kwa kuzipa Uhuru na mipaka ya
kazi taasisi au idara zote zilizopo ndani ya klabu.
Anawakumbusha
wadau kurejea azimio la Bagamoyo ambapo Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA)
lilileta utaratibu wa kutoa leseni kwa klabu zilizotimiza mashari.
Anasema masharti
yanayotajwa yakiwemo kuwa na utawala bora, timu za vijana n.k kama
yatazingatiwa, klabu nitakuwa katika nafasi nzuri ya kuchagua mfumo wa
kujiendesha kama ni wa wanachama au wanahisa.
CHARLES NDAKI, Mtaalam wa Masuala ya Masoko
Ndaki anasema
jina la timu (brand) ni rasilimali muhimu inayitakiwa kutunzwa na kuendelezwa
kwa sababu ndio msingi wa biashara iliyopo katika soka.
Anasema klabu
zinatakiwa kuweka mikakati ya kujipa upekee ili kujitofautisha na wengine kwa
lengo la kutumia vizuri jina lake kibiashara.
Anasema kwa
kufanya hivyo klabu itakuwa na wigo mpana wa wanachama na mashabiki (fun base)
NA hivyo kuwa na uwezo mkubwa wa kufanya biashara kupitia jina la klabu.
MICHAEL WAMBURA -
KATIBU WA ZAMANI WA TFF
Wambura anasema
serikali ndio inayoweza kulinda maslahi ya wengi katika mabadiliko haya hivyo
watumie vyombo vyake kuhakikisha yanafanyika mabadiliko yenye maslahi kwa walio
wengi.
Anasema ni vyema
mabadiliko yakafanyika kwa kuzingatia Sheria za nchi, TFF, CAF na FIFA hivyo
aliviomba vyombo vinavyohusika, TFF, BMT na Wizara kuhakikisha zinawezesha
mabadiliko haya kwa manufaa ya klabu, wanachama, wawekezaji na sekta ya michezo
kwa ujumla.
HENRY TANDAU MKUFUNZI WA FIFA
Anasema wadau
katika mabadiliko haya lazima wajifunze mifumo minne ya kuendesha soka kablaya
kuelekea mabadiliko.
Anaongeza tatizo
kubwa la wadau wa michezo hawapendo kujifunza wanaendesha klabu kwa mazoea.
Anasema biashara
ya mpira ni ya aina yake kwa sababu ili ufanikiwe inahitaji ushirikoane na
mshindani wako. Kutokana na upekee huo, biashara hii inatakiwa kuendeshwa na
wataalamu wenye weledi nayo.
Anasema Azimio la
Bagamoyo ndio lilitakiwa kuwa msingi mkubwa wa mabadiliko kwa sababu limeanisha
vitu vingi vizuri ambavyo havijafanyiwa kazi.
Anaongeza kuwa
japo tumechelewa lakini tulipofika tungeanza na Azimio la Bagamoyo kuelekea
kwenye mabadiliko ya kweli.
JAMAL RWAMBOW, MJUMBE WA BARAZA LA MICHEZO LA TAIFA (BMT)
Anasema
mabadiliko haya hawawezi kufanyika bila kuishirikisha serikali. "Itakuwa
ni kujidanganya kuamini kwamba wawekezaji na wanachama wanaweza kufanya
mabadiliko haya bila kuishirikosha serikali kwa sababu serikali ndio baba"
anasema Rwambow.
Alitoa mwito kwa
wadau kuishirikisha serikali na hasa kufuata maelekezo yaliyotolewa na BMT
kuhusiana na utaratibu wa kufanya mabadiliko hayo kama klabu zi nataka kuelekea
huko.
Mwishowe Katibu
Mkuu wa TASWA, Amir Mhando aliahidi kwamba chama chake kitashirkiana wadau
mbali mbali kuhakikisha makongamano kama hayo yanafanyika Mara kwa mara ili kutoa
fursa kwa wadau ya kujifunza.
COMMENTS