TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI * COTU –Kenya yasema wanatamani Rais Magufuli aende kwao kwa mwaka mmoja WAZIRI MKUU Kassim M...
TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI
* COTU
–Kenya yasema wanatamani Rais Magufuli aende kwao kwa mwaka mmoja
WAZIRI MKUU Kassim
Majaliwa amesema Serikali haitawavumilia waajiri ambao hawatoi mikataba ya
ajira kwa wafanyakazi wao na amewaonya waache tabia hiyo mara moja.
“Nitoe wito kwa waajiri
wote ambao wamekuwa na tabia ya kutokutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi
wao, waache tabia hiyo mara moja, kwani Serikali haitamvumilia mwajiri wa namna
hii,” alionya.
Ametoa agizo hilo leo (Jumatano,
Novemba 23, 2016) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Sita wa Shirikisho la Vyama
vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) katika ukumbi wa Mwalimu Julius K. Nyerere
ulioko Chuo cha Mipango, nje kidogo ya mji wa Dodoma.
Akijibu hoja ya waajiri
kutokutoa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi ambayo iliibuliwa kwenye risala
yao, Waziri Mkuu amesema kifungu cha 14 cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini
Na. 6 ya mwaka 2004 kinaelekeza aina mbalimbali za mikataba
inayotakiwa kutumika kuajiri wafanyakazi. “Kisheria mwajiri anao wajibu wa
kuhakikisha kila mtumishi wake ana mkataba wa kazi kwa maandishi,”
alisisitiza.
“Pia ninawaagiza maafisa
wa kazi wanaohusika na kaguzi za kazi kote nchini, wahakikishe kila mwajiri
anafikiwa wakati wa ukaguzi na hatua stahiki zinachukuliwa kwa wote
wasiotekeleza matakwa ya Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini,”
alisisitiza.
Alisema mkataba wa ajira
ni haki ya mfanyakazi na ndiyo ufunguo wa mahusiano mema yanayoweza kuleta
utulivu, amani, kuongeza tija na uzalishaji sehemu ya kazi.
Akijibu hoja kuhusu
wafanyakazi kuwekwa ndani kiholela, kunyanyaswa, kushushwa vyeo na kusimamishwa
kazi na wanasiasa, Waziri Mkuu alisema Serikali
chini ya uongozi wa Dkt. John Pombe Magufuli itaendelea kuzingatia utawala wa
sheria na kanuni za utawala bora ili kuhakikisha kuwa haki za wafanyakazi
zinalindwa ipasavyo.
”Kimsingi watumishi
wanasimamiwa na mamlaka za kinidhamu na sheria mbalimbali ambazo hazina budi
kuangaliwa kwa pamoja kabla ya kuchukua hatua. Ninawaagiza viongozi wenzagu wa
kisiasa na walioko katika wizara na taasisi zote za Serikali, mikoani,
wilayani, kwenye idara za Serikali na Halmashauri wazingatie utawala wa sheria
wakati wa kushughulikia masuala mbalimbali yanayohusu wajibu na haki za
wafanyakazi,” alisema huku akishangiliwa.
Risala yao iligusa maeneo
mengine kama vile watumishi wa umma kutopandishwa vyeo kwa wakati muafaka;
walitaka kujua bodi za mishahara za kisekta zitaanza kazi lini; kukosekana
kanuni za uandikishwaji wa vyama vya wafanyakazi na waajiri; marekebisho ya Mifuko
ya Hifadhi ya Jamii na ucheleweshwaji wa malipo ya pensheni; haja ya kuoanisha
Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002 na Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini
ya mwaka 2004.
Akijibu baadhi ya hoja hizo,
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu, Bunge, Kazi Ajira na
Vijana) Bibi Jenista Mhagama alisema dhana ya utatu baina ya wafanyakazi,
waajiri na Serikali ndiyo nguzo kuu ya kukuza uchumi wa Tanzania.
Akifafanua kuhusu fao la
kujitoa, Waziri Mhagama alisema baada ya uongozi wa TUCTA kukamilika, itabidi
wakutane na kukaa pamoja kuainisha sera inataka nini na hali ya uchumi ya sasa
ikoje huku wakiangalia dhana nzima ya hifadhi ya jamii nayo inataka nini.
“Kuna haja ya kuangalia
sera inataka nini, tunapaswa tuangalie mabadiliko ya kiuchumi katika nchi yetu
na kutazama dhana nzima ya hifadhi ya jamii kwenye maisha yetu ya uzeeni.
Tukikaa pamoja, yaani, mwajiri, mfanyakazi na Serikali, tutapata njia ya
kisheria ya kuweza kulifunga jambo hili ili lisiendelee kuwa kero kwa
wafanyakazi wetu,” alisema.
Akijibu hoja kuhusu
suala la watumishi kutopandishwa vyeo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utumishi
na Utawala Bora), Bibi Angella Kairuki alisema kwa kipindi cha miaka mitano
jumla ya watumishi 343,689 walipandishwa vyeo ikiwa ni kuanzia mwaka 2011 hadi
2016. Hata hivyo, alisema wanakabiliwa na changamoto ya watumishi wengine
kutokidhi vigezo.
“Kuna baadhi ya watumishi
hawakidhi vigezo vya maendeleo na masharti vya muundo wa masharti ya utumishi
wa umma. Tumetoa maelekezo kuwa wale waliokosa vigezo na wamekaa muda mrefu
bila kupandishwa vyeo, wapewe mafunzo na bajeti zitengwe ili waweze kutimiza
vigezo vya muundo wa utumishi wa umma,” alisema.
Katika hatua nyingine, Katibu
Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini Kenya (COTU), Bw. Francis
Atwoli alisema anaikubalia kasi ya Rais Magufuli katika kupambana na rushwa na
kuwataka Watanzania wamuunge mkono badala ya kulalamikia kasi kwani wao
wanatamani mwakani aende kugombea kwao katika uchaguzi mkuu ujao.
“Ninawasihi wanaTUCTA suala
la rushwa msilipe nafasi. Mpambane nayo kwa sababu kule kwetu imeota mizizi.
Muungeni mkono Rais Magufuli, badala ya kulalamika kuwa kasi yake ni kubwa mno.
Mnasema eti ana spidi sana, mkiona taabu mtuazime japo kwa mwaka mmoja ili aje
atunyooshee mambo kule kwetu,” alisema huku akishangiliwa.
Aliwataka wahimize
uhusiano uliopo baina ya vyama vya wafanyakazi, waajiri na Serikali iliyopo
madarakani na kuwataka wadumishe umoja miongoni mwa viongozi na wanachama
mara baada ya kumalizika kwa uchaguzi.
“Msiruhusu mgawanyiko wa
makundi baada ya uchaguzi sababu hauwasadii wafanyakazi ambao ni wanachama
wenu. Mmeona madhara ya kuendeleza makundi kule nchini kwetu, msiruhusu hayo
yatokee hapa,” alionya.
TUCTA inatarajiwa kufanya
uchaguzi wake kesho (Alhamisi, Novemba 24, 2016) na kuchagua uongozi mwingine
utakaongoza kwa kipindi cha miaka mitano. Uchaguzi wa mwisho ulifanyika 2011.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
DODOMA.
JUMATANO, NOVEMBA 23,
2016.
COMMENTS