SERIKALI imewasilisha bungeni kwa mara ya pili Muswada wa Huduma za Habari wa mwaka 2016 ukiwa na mabadiliko katika maeneo saba ikiwemo k...
SERIKALI
imewasilisha bungeni kwa mara ya pili Muswada wa Huduma za Habari wa mwaka 2016
ukiwa na mabadiliko katika maeneo saba ikiwemo kuviondolea vyombo vya habari adhabu
kwa baadhi ya makosa ya mwandishi na ukamataji wa mitambo na vifaa vya
wanahabari.
Aidha,
Serikali imewatoa hofu waandishi kuhusu muswada huo na kusema ikiwa waandishi
wa habari watasimamia maadili yao na kutii sheria, hawana haja ya kuhofu kwani
Serikali itakuwa mlinzi wao namba moja.
Muswada
huo ukiwa na maboresho, uliwasilishwa jana na Waziri wa Habari, Sanaa,
Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye.
Wakati Serikali ikieleza hayo, Kambi Rasmi ya Upinzani
bungeni inayohusika na habari, imeupinga Muswada huo na kueleza kuwa unakuja
kuua na kuzika kabisa haki na uhuru wa kupata habari kwa wananchi, kuwafunga
wahariri na waandishi na umelenga kusambaratisha kabisa tasnia ya habari.
Msemaji
wa Kambi hiyo bungeni, Joseph Mbilinyi, katika hotuba yake jana, alishauri
Waziri mwenye dhamana ya habari asiachiwe mamlaka ya kuweka viwango vya elimu
katika kanuni bali Bodi ya Ithibati na Baraza Huru la Habari likaweka viwango
hivyo. Ilipendekeza kiwango kiwe diploma.
Kambi hiyo ilitaka Bodi ya Ithibati isiishie kwa waandishi
wa habari bali pia iwe na mamlaka ya ithibati kwa elimu inayotolewa na vyuo
mbalimbali vya uandishi wa habari nchini.
Mbilinyi
alipendekeza kuwepo kifungu mahsusi cha kuwalinda wanahabari dhidi ya vitendo viouvu vinavyoweza
kufanywa dhidi yao na kuzungumza kuhusu
habari za uchunguzi ambazo alidai umeziua kabisa.
Hata hivyo kambi hiyo ya upinzani iliunga mkono kuanzishwa
kwa Bodi ya Ithibati pamoja na Baraza Huru la Habari ili kuwe na viwango na
uangalizi pamoja na uratibu wa kitaaluma katika tasnia ya habari pamoja na
kuwakatia bima waandishi wa habari.
Aidha, Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, kuhusu
muswada huo, imependekeza pamoja na uvaaji wa vitambulisho kwa waandishi wa
habari, kanuni zieleze kuhusu mavazi kama ilivyo kwa wanasheria, madaktari na
wauguzi. Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Peter Selukamba, ndiye aliyetoa maoni ya
kamati hiyo bungeni jana.
Maboreshi saba:
Nape
alisema walifanya maboresho kwa kuzingatia mawazo ya wadau ikiwemo Kamati ya
Bunge, taasisi za habari kama Jukwaa la Wahariri (TEF), Baraza la habari (MCT),
Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
(LHRC), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa), Taasisi ya Wanahabari
Kusini mwa Afrika, Tanzania (MISA-TAN) na Umoja wa Wamiliki wa Vyombo vya
Habari (MOAT)
Waziri
Nape pamoja na kueleza kuwa muswada huo uliopigwa danadana kwa zaidi ya miaka
23 utaleta mapinduzi na kuweka historia katika tasnia ya habari nchini,
alieleza maboresho kadhaa.
Maboresho
hayo ni katika eneo la kuanisha haki na wajibu wa wanahabari; kuainisha haki ya
chombo cha habari kukata rufaa; uwakilishi wa wanahabari katika Bodi ya
Ithibati; Jaji Mkuu kuweka utaratibu kusikiliza haraka kesi za kashfa.
Maeneo
mengine ni kuviondolea vombo vya habari adhabu kwa baadhi ya makosa ya
mwandishi; vyombo vya dola kukamata mitambo na vifaa vya wanahabari na mitambo
kutohusika moja kwa moja kwa kosa la gazeti.
Akifafanua
kuhusu maboresho hayo, Nape alisema kuhusu haki ya wanahabari lazima kuzingatia
mikataba ya kimataifa ambayo nchi imesaini na kuridhia pamoja na matakwa ya
Kikatiba.
"Muswada
sasa umeweka mfumo wa wazi zaidi na wa kidemokrasia ambapo uamuzi wa Mkurugenzi
wa Idara ya habari-Maelezo hautakuwa wa mwisho. Chombo husika kinaweza kukata
rufaa kwa Waziri wa Habari na kisiporidhika na uamuzi kinaweza kupinga suala
hilo mahakamani," alisema Nape.
Nape
alisema katika uwakilishi wa Bodi ya Ithibati, kati ya wajumbe saba, wakiwemo
wanne waandishi, sasa kutakuwa na uwiano katika sekta binafsi ya ya umma. Awali
hakukuwa na uwiano huo.
Kuhusu
kusikiliza kesi za kashfa kwa haraka, Nape alisema Jaji Mkuu kwa kuzingatia
tathimini ya uwezo wa mahakama na rasilimali, na kama ilivyo kwa kesi nyingine
za uchaguzi na za biashara, atatunga kanuni zitakazoweka muda wa kumalizika kwa
kesi. Awali muswada haukueleza hilo.
"Moja
ya mageuzi makubwa ya muswada ni kuviondolea vyombo vya habari au umiliki wake
adhabu ya makosa yanayomuhusu mwandishi binafsi. Sasa mwandishi kama
mwanataaluma kamili anaweza kuwajibishwa na Bodi ya Ithibati kwa makosa ya kimaadili
badala ya mtindo wa sasa wa kila kosa la mwandishi kubebwa na chombo
chake," alisema Nape.
Kuhusu
kukamata mitambo, Nape alisema maoni ya wadau yamezingatiwa na sasa mamboresho
yamemuondoa Mkurugenzi wa Idara ya Habari kuwa na mamlaka ya kukamata mitambo
badala yake kazi hiyo itafanywa na Polisi kwa mujibu wa Sheria ya Makosa ya
Jinai (CPA).
Aidha,
Nape alisema kuhusu mitambo ya uchapishaji kuwa sehemu ya makosa chombo cha
habari kinapoandika uchochezi au makosa mengine ya kashfa, wachapaji wameondolewa
katika makosa yanayotokana na maudhui ya watu wengine.
Muswada
huu unajadiliwa kwa siku mbili, jana na leo bungeni, utapitiwa kifungu kimoja
baada ya kingine, kabla ya kupitishwa.
Source: HabariLeo
COMMENTS