Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amemshukuru Rais Dk Johna Magufuli kwa kipindi cha mwaka mmoja alichomuami...
Waziri wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amemshukuru Rais Dk Johna Magufuli kwa
kipindi cha mwaka mmoja alichomuamini kutumikia wizara hiyo kama kijana.
Nape alisema hayo LEO jijini Dar es Salaam mbele ya Kanisa la
Mtakatifu Peter ambako alikwenda kukutana na waandishi wa habari kwenye hoteli
ya Protea hata hivyo mkutano huo kuzuiwa na jeshi la polisi hivyo kulazimika
kuzungumza akiwa juu ya gari.
“Lengo la kwangu la
kuja hapa la kwanza ilikuwa ni kumpongeza Rais kwa uamuzi alioufanya na pia
kumshukuru kwa kuniamini kwa mwaka mmoja, na wale mliotumwa sikilizeni
mkawaambie,” alisema Nape.
Alisema anamshukuru Rais alimuamini kama kijana na kumpa
heshima ya kuingia kwenye baraza la mawaziri na kwamba kama ambavyo Rais alimuamini
atumikie kwenye nafasi hiyo lakini sasa ameona na amemuweka Aliyekuwa Waziri wa
Katiba na Sheria Dk Harrison Mwakyembe.
Nape alisema anapongeza pia Dk Mwakyembe na pia anamuunga
mkono kwa uteuzi huo na kwamba kwasababu
ni mwanahabari anaimani atasimamia vizuri tasnia hiyo.
Nape alisema hana kinyongo na Rais Magufuli katika uamuzi wake
alioutangaza asubuhi jana wa kumteua Dk Mwakyembe kuwa Waziri wa wizara hiyo ambayo
alikuwa akiiongoza yeye kushika nafasi yake.
“Kama ambavyo sikumshawishi Rais kunichagua ndivyo ambavyo
sina say (kauli) na uamuzi aliofanya, lakini wakati anaunda baraza walikuwepo
watu wengi sana, alipoamua kunichukua mimi kuna watu walikuwepo na walikubali,
mimi leo nakatalia nini, sina sababu ya kukataa,” alisema Nape.
Baada ya Gari ya Nape kufika eneo la kanisa hilo wakati
akishuka, alitokea mtu ambaye alianza kumsukuma Nape akimrudisha kwenye gari
asishuke kwenda kuzungumza na waandishi wa habari ambao walikuwa wamejaa katika
eneo hilo na baadaye kuja askari waliokuwa na sare.
Kitendo hicho cha Nape kusukumwa arudi kwenye gari na mtu yule
aliyekuwa na nguo za kiraia ambaye Nape alisema hamfahamu na hajui ametumwa na
nani Nape aliendelea kusisitiza kuwa hakuna haja ya kutumia nguvu na silaha
akimtaka amuache aendelee kuzungumza na wanahabari.
Kutokutii huko kwa Nape kulimfanya mtu huyo ambaye alikuwa
akimsukuma kulazimika kutoa silaha (bastola) akisisitiza Nape arudi kwenye
gari.
Baada ya mvutano wa muda mrefu, Nape aliamua kusimama kwenye
mlango wa gari na kuanza kuzungumza na wanahabari akiwa hapo na baadaye kuingia
kwenye gari kufungua dirisha la juu ya gari akatoa kichwa na kuanza kuzungumza
akiwa hapo huku wale watu waliokuwa wakimzuia wakiendelea kuwepo pale.
Katika mazungumzo yake na wanahabari, Nape alisema amejitahidi
kutimiza wajibu wake katika nafasi yake ya uwaziri.
“Jana wakati nilipoongea na vyombo vya habari wakati napokea
ile ripoti, nilisema kuna gharama ya kulipa wakati wa kusimamia haki za watu na
mimi niko tayari kulipa, sioni sababu kwanini vyombo vinapaniki,” alisema Nape
na kuongeza kuwa uzalendo wake kwa nchi
hauwezi kutiliwa mashaka
“Nimekuwa mzalendo kwa nchi yangu, nimekuwa muungwana kwa nchi
yangu na ninaapa kuendelea kuwa muungwana kwa nchi yangu hilo hakuna
atakayelibadilisha,” alisema.
Alisema amekuwa pia mzalendo kwa CCM chama ambacho kiko kwenye
shimo alisimama kukiinua uzalendo ambao haufai kutiliwa mashaka na kwamba alijifunza
usemi wa ‘nitasema kweli daima fitina kwangu mwiko’ na alichokisimamia ni
kusema kweli.
Alisema aliwataka watu hao waliokuwa wakimzuia pamoja na watu
waliowatuma wasihangaike naye kwani ni mtu mdogo kuliko Tanzania badala yake
wahangaike na mambo mengine yenye manufaa kwa nchi.
“Nimekuja hapa mtu anakuja na bastola ananiamrisha nirudi
kwenye gari, nani amekupa mamlaka hayo, unalipwa kwa kodi ya kwetu, mnajua ni
namna gani tumepambana kwaajili ya nchi hii, miezi 28 nalala porini angalieni
mkono wangu huu,” alisema Nape.
Nape alisema hayo akionesha mkono ambao aliumia baada ya
kupata ajali ya gari … ambapo alisema pia kuwa alipigana kuhakikisha Chama cha
Mapinduzi (CCM) kinabaki madarakani.
Nape alisema vyombo vya ulinzi na usalama viangalie jambo hilo
lililofanyika la kumzuia kushuka kwenye gari kwa kutumia nguvu na kummtolea
bastola wakati hakuwa na nia mbaya.
“Nia yangu haikua mbaya kwa serikali yangu, nia yangu ilikuwa ni
kuwaeleza watanzania kwamba maisha lazima yaendee, sasa wanapokuja watu
wachache (wapuuzi) wanadhani wanaweza kukoroga hivi mambo,” alisema.
Alisema alipoteuliwa Rais John Magufuli hakumuuliza hivyo
wakati anataka kumuweka mtu mwingine hana sababu ya kuulizwa na pia hana
kinyongo na Rais.
“Sijasema chochote kwamba nina kinyongo na Rais wangu, kwani
kuna watu wanataka wao ndio wawe waamuzi wa mawazo ya vijana wa nchi hii,”
alisema Nape.
Aidha alisema kinachowakutanisha watu sio sare za CCM za rangi
ya kijani bali imani ya kuwa wakweli kuachana na fitina.
Alisema uzalendo amefundishwa na baba yake marehemu Moses
Nnauye ambaye alikuwa mwanasiasa mkongwe wa CCM kusema kweli na kusimamia
anachokiamini na kama kitaleta matatizo hana shida kwani alishawahi kufukuzwa
kwenye chama chake hicho.
Nape ambaye alishawahi kufukuzwa CCM alisema katika maisha ya
siasa kupita kwenye migogoro ni jambo la kawaida kwani lazima mbegu ioze ndipo
iote, “sasa mbegu niliyoipanda itaota, mbegu ya kusimamia haki hakika itaota.”
Aliwaasa vijana kusimamia ukweli, kutokuwa waoga na kusimamia
kile wanachokiamini.
Nape alisema katika kipindi ambacho amekuwa katika wizara hiyo
anaamini ametumia akili na uwezo wake wote kuwatumikia watu walioko chini na
wizara hiyo na kwamba alipata ushirikiano wa kutosha.
“And I real love you people, napenda kufanya kazi na nyie na
nimefurahi sana, sana kufanya kazi na nyie, na nina waombeni mumuunge mkono
waziri mpya aliyepewadhamana na fanyeni nae kazi na pia endeleeni kumuunga
mkono Rais Magufuli ndie rais tuliyepewa na Mungu na tuliyempigia debe
watanzania,” alisema.
Aliwataka pia watanzania kuendelea kudumisha umoja na
mshikamano wan chi na kwamba sio wakati wa kuvuruga nchi kwani kuna mambo
mazuri mbele. lisema alipenda kuendelea kufanya kazi hiyo lakini wakati umefika
amelazimika kuondoka
Nape alisema anarudi kufanya kazi katika jimbo lake kwa
kuwatumikia katika yale waliyomtuma kama mbunge wao.
COMMENTS