Na abdul mtemvu Ulimwengu wa siasa ulimalizika mwaka 2016 kwa kituko kikubwa cha aliekuwa rais wa Gambia, Yahya Jammeh, kwanza kuku...
Na abdul mtemvu
Ulimwengu wa siasa ulimalizika
mwaka 2016 kwa kituko kikubwa cha aliekuwa rais wa Gambia, Yahya Jammeh, kwanza
kukubali uchaguzi halali wa kidemokrasia kufanyika nchini kwake (hakulazimishwa
na mtu yeyote). Ukafanyika na akashindwa
kihalali na, baadae mwenyewe, kumpongeza
aliemshinda (Adama Barrow), na dunia ikampongeza kwa kuwa muungwana wa kukubali
matokeo. Dunia ilimpongeza kwa, pengine, kufikiria Afrika imejiingiza kwenye
Ulimwengu wa demokrasia ya Kimagharibi. Kumbe sio! Yaliyotokea na kumkuta Yahya
Jammeh ni historia, tofauti na heshima ambayo, pengine, angeipata kwa kukubali
kwake kushindwa na kupata heshima iliyotukuka.
Mfano wake
ni sawa na ule wa nchi ya Burkina Farso, ambayo iliinggia kwenye heka heka na misuko
suko ya kijinga tu kwa Blaise Campaore kutaka kung’ang’ania madaraka! Sawa na yalioikumba
Ivory Coast. Kisa, eti, ni wapambe na
ndugu hata marafiki walio karibu na kiongozi mhusika ambao hawako tayari kurudi
kijiweni ilhali kuna lukuki ya wananchi wako kijiweni! Hawa ndio chimbuko la
vurugu na machafuko yote! Wapambe nuksi. Nani asiejua Bagbo kaponzwa na nani?
Alishindwa uchaguzi halali wa kidemokrasia nchini kwake na, baada ya kushindwa,
akashawishiwa na mkewe kuitumbikiza nchi
yake kwenye machafuko makubwa ambayo hayana mithili. Leo, yuko wapi? Hadithi kwa Afrika inaendelea na hakuna
anaejifunza hadi kiyama kitukute.
Blaise Campaore
(aliyempindua mwanamapinduzi wa mfano barani afrika na swahiba wake wa damu –Tomas
Sankara),baada ya kunogewa na madaraka baada ya miaka takriban ishirini na saba
madarakani akakataa kuachia ngazi, huku
akitaka kushawishi bunge kubadili katiba ili aendelee na uongozi wake usio na
tija kwa nchi yake. Ya, Yahya Jammeh
ndio yalikuwa ya Blaise Campaore na ndio yaliyokuwa ya Bagbo! Hakuna
aliejifunza kwa mwenzake?
Hawa ndio viongozi wetu
wa bara letu ambao, kwa kiwango kikubwa, wengi wao wamechukua nafasi ile ile ya
waliokuwa wakoloni wetu kupora rasilimali za nchi na, bila aibu, kuzipeleka kule kule Ulaya! Neno demokrasia kwao ni
msamiati tu usio maana wala tafsiri inayoeleweka. Demokrasia kwao ina tafsiri
ya wao kuwepo madarakani, ama iwe kwa hila au ghilba. Alimradi na ikibidi
wang’oke basi itakuwa ni kwa mbinde. Tena mbinde kweli kweli (wakati mwingine
mpaka wazungu wawalazimishe). Kwao haijalishi madhara ama madhira gani wanasababisha
kwa wananchi na nchi zao.
Aliekuwa rais wa awamu
ya nne, Dk Jakaya Mrisho Kikwete, aliwashangaza mabalozi na wawakilishi wa Afrika,
nchini China, wakati wa ziara yake nchini humo, alipozungumza kuhusu kuchoshwa
na Urais na kutamani walau muda wake ungekuwa umeisha ili arudi nyumbani kuwa
mtu wa kawaida! Rais Kikwete alizungumza hayo wakati hata muda wake wa mihula
miwili ya miaka mitano mitano haijaisha rasmi. Wakati wa kuadhimisha miaka 53
ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, Tanzania na Dunia ilishuhudia viongozi
wastaafu wa Tanzania (Mzee Mwiyi, Mkapa, Kikwete na Karume) wakiwepo kwenye
membari wakicheka na kufurahi. Nchi gani Afrika ambayo ina viongozi wastaafu wanaoweza kuwepo pamoja
kwenye hafla ya kitaifa wakawa hawana bifu miongoni mwao? Wanacheka tu!
Blaise Campaore, kama
mwenzake Yahya Jammeh, alikaribia
kumaliza miaka ishirini na saba ya utawala ambao wangalau ulikuwa na chembe
chembe za kidemokrasia pamoja na kuwa alikuwa akiipinda pinda, baada ya awali
kuingoza nchi yake kijeshi, lakini ni wazi kwa tamaa yake hiyo, miaka yote hiyo
hayakumtosha. Angetaka, si angefanya katiba ya kuwa kiongozi wa maisha! Nani
angeweza kumzuia, lakini hakuelewa. Hakuelewa kuwa katiba ndio imemponza.
Katiba haichezewei chezewi kama kutafuna tambuu.
Hata hivyo, hii sio
hoja ya msingi. Hoja ya msingi ni kwamba, kaifanyia nini nchi yake na watu wake
miaka yote hiyo? Alimpindua Tomas Sankara (kama mwenzake Yahya Jammeh
alivompindua kiongozi halali), lakini ilikuwa yeye afanye nini? Ni wazi kuwa kilichompelekea
kumpindua, na hatimae kumuua, rafiki yake na mwanamapinduzi mwenzake ni wivu na
uchu wa madaraka. Hakusukumwa na mwamko kuwa mapinduzi yale, chini ya kapteni
Sankara, yalikuwa yamekosa mwelekeo na kuwa Sankara alishapoteza dira na, kwa
hali hiyo, akajiona yeye ndio alifaa kurekebisha mambo.
Hata pale alipomuua
mwenzake dunia ilimsamehe. Viongozi wenzake wa Afrika (wakati ule hata Mwalimu
Nyerere alimsamehe), waliangalia pembeni wakidhani, pengine, ni ajali ya
kisiasa ambayo hutokea nyakati za vugu vugu za mapinduzi. Kumbe hakuwa na Uanamapinduzi
wowote! Uchu na tamaa za madaraka ndizo zilizotawala udhalimu wake.
Ni kwa nini viongozi
wetu (wa Afrika) hawaheshimu katiba? Ni kwa nini wanafikiri wananchi wao ni
kundi sawa na la kondoo la kuburuzwa buruzwa tu, kundi la kudanganywa danganywa
kila mara na wao ndio waamuzi wa mwisho wa mustakabali wa taifa na watu wao?
Kama Blaise Campaore na Yahya Jammeh wameshindwa kuipa msukumo wa maendeleo nchi
zao badala ya kujitajirisha wao, jamaa na familia zao tu, kwa miaka yote waliokaa
madarakani, wangeweza kufanya nini kwenye miaka mingine wanayotaka kujiongezea
- hata kama wangekaa daima madarakani.
Nchini Burkina Faso, na
baadhi ya nchi zinazofanana nayo, wakati wa Campaore, wananchi wa Ufaransa na wageni wengine waliishi
maisha ya peponi kuliko hata Waburkinabe wenyewe ambao wengi wao wakilindwa na
vikosi vya jeshi maalum la Ufaransa huku vijana (wasomi wa Kiburkinabe) wakiwa
hawana matumaini yoyote ya hatma za maisha yao ya siku hadi siku. Maisha yasio
matarajio ya ahueni kwa leo wala kesho! Huu na hii ndio dhana ya uhuru wa
baadhi ya nchi zetu barani Afrika! Maisha na hali ambapo viongozi wamekua sawa
na mwewe wanaovizia na kutafuna vifaranga vya kuku. Wanachuma utajiri unaoishia
nchi za Ulaya. Kwao, wananchi wao ndio vifaranga na wao ndio mwewe!
Tony Blair,
wakati akiwa madarakani, aliwahi kukaririwa akisema, kwamba: ‘Africa is not
poor but is poorly governed’ dhana ambayo haina ubishi kwa kuwaangalia aina ya
viongozi wengi barani kwetu. Kwa hakika, tumefika mahali, wazungu tunaowaenzi
sana wamewafanya viongozi wetu wengi kuwa kama wanasesere wao! Nchi yoyote
Afrika ambayo balozi wa Ulaya akiletwa na akikaa miaka miwili ndio anaishia
kuwa mtaalam wa mambo ya Afrika nchini kwao. Ni aibu! Bongo tuna watu wamekaa miaka hata
ishirini vijijini wakiwa viongozi, lakini hatuna hata mtaalam mmoja ambae
kaandika kitabu cha changamoto ya Wilaya ua Kijiji alichokiongoza! Mzungu
anakuja nmiaka miwili tu, lakini mwaka mmoja tu anatoa darasa kwao! Anajiita
mtaalam na hata kutufundisha sisi wenyewe wenye nchi yetu.
Hakika, tufike mahali
viongozi wetu wabadilike. Kama mifumo ya kigeni imetushinda, basi, turudi ama
tubuni mifumo itakayoendana na tamaduni na historia zetu. kwani kuna ulazima
gani, mathalan, kuwa na vipindi vitano vitano vya mihula miwili vya Urais? Kwa
nini tusifanye miaka kumi kumi ya vipindi viwili ili kiongozi atosheke ama hata
kipindi cha muhula mmoja wa miaka kumi na ushee ya rais kutawala angalau
atosheke yeye na wapambe wake? Mbona Papa, Kadinali au Mufti hawana muhula wa
uongozi? Akitawazwa ni mpaka umauti umfike ndio aje mwingine.
Ili balaa la viongozi
wetu kutaka katiba iseme mihula ya utawala katuletea nani wakati hatuiheshimu?
Iweje, viongozi wetu wanaoridhia balaa hili la kutaka mihula ndio hao hao wawe chanzo
cha machafuzi ya nchi zetu? hakika, ipo haja ya kutafakari ili.
Wasalaam.
COMMENTS