Mkuu wa Shule ya St. Joseph Cathedral, Sista Theodora Faustine akimkabidhi zawadi na cheti, Prof. Rwekaza Mukandala ambaye alikuwa mgen...
*Asema utu,
maendeleo na maisha bora havipatikani kwa fedha
MAKAMU MKUU wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Prof.
Rwekaza Mukandala amewataka vijana wanaohitimu kidato cha sita nchini wawe
makini na wasikubali kusombwa na mawimbi ya dunia.
Ametoa wito huo jana (Jumamosi, Mei
14, 2017) wakati akizungumza na wahitimu 237 wa kidato cha sita wa shule ya
sekondari ya St. Joseph Cathedral kwenye mahafali ya sita ya shule hiyo
yaliyofanyika shuleni hapo, jijini Dar es Salaam.
Prof. Mukandala alisema: “Kwa hatua
mliyofikia kila mmoja anapaswa atafakari kwa kina wito wake kimaisha. Kuweni
makini, msisukumwe na mawimbi ya dunia na kujikuta mmepoteza ndoto zenu,”
alisisitiza.
“Kuhitimu kidato cha sita si jambo
dogo. Ni hatua ya kuwaongiza kujiandaa na utu uzima ikiwemo kujiunga na elimu
ya vyuo vya juu na kuingia kwenye ndoa. Ni muda wa kutathmini yale uliyopitia
na kutafakari maisha yako ya baadaye. Ni fursa ya kutoa shukrani kwa Mungu, kwa
wazazi na walimu ambao walifanya kazi kwa umakini na kujitoa ili mfikie hatua
nzuri mliyopo sasa,” alisema.
Alisema kuanzia sasa kila mmoja wao
anapaswa kujiamini, kujituma zaidi na kujiona kuwa ana wajibu wa kujiletea
maendeleo binafsi. “Mnapaswa kuepuka mwenendo wa kujiona mnyonge, au mtu
asiyeweza kutimiza ndoto zake. Jenga tabia ya kuwa makini na maisha yako, jali
mazingira yako na maendeleo yako,” alisisitiza.
Aliwataka wahakikishe wanakuchukua
hatua mahsusi na kupata taarifa sahihi kuhusu taaluma wanazozitaka. Aliwataka
wawe waadilifu na wenye heshima kwa watu wote lakini pia akawaasa juu ya maisha
ya kutaka kupata fedha kwa haraka na kujilimbikizia mali.
“Epukeni rushwa na ufisadi.
Mnatakiwa kujua kuwa utu, maendeleo na maisha bora havipatikani kwa fedha
ingawa nayo ni muhimu katika maisha. Msitegemee kuishi kwa kuzingatia mambo
makubwa yanayopimika kwa fedha,” alisema.
Akitoa mfano, Prof. Mukandala
alisema: “Msikimbilie kuwa na magari mengi bila kujua nani atayatumia, au
kujenga nyumba kubwa bila kujua nani atahitaji nafasi hiyo kubwa. Unanunua simu
mbili au tatu bila kufikia athari zake kwa afya na mahusiano yako. Kabla
hujachukua hatua ni lazima ujiulize, je unakihitaji kitu hicho? Kuweni makini
na matumizi ya fedha badala kujilimbikiza vitu vya anasa,” alisema.
Aliwataka wazazi waendelee kuwalea
vema vijana hao kwa sababu bado wanahitaji usimamizi wa wazazi kwa kila hatua
wanayosonga mbele. “Tuendelee kuwaunga mkono watoto wetu kwa sababu jukumu letu
kama wazazi bado liko palepale,” alisema.
Mapema, akimkaribisha
mgeni rasmi kuzungumza na hadhira iliyokuwepo, Mkuu wa Shule ya St. Joseph
Cathedral, Sista Theodora Faustine alisema St. wanafunzi waliohitimu jana ni
237 ambao kati yao wavulana ni 140 na wasichana ni 97 waliokuwa wakichukua
michepuo ya ECA, EGM, CBG, HGE, HGL, PCM, PCB na PGM.
Alisema anaamini kwamba wahitimu
wote watakuwa na sifa za kujiunga na vyuo vikuu mwaka huu kwa sababu shule hiyo
imekuwa ni ya kwanza yenye wingi wa ufaulu kuliko shule yoyote mkoani Dar es
Salaam. “Tumekuwa tukipata wanafunzi bora kitaifa mara kwa mara na mwaka jana
tulipata wanafunzi bora kutoka michepuo ya PCB na ECA,” alisema.
Sista Theodora alisema wamekuwa
wakifaulisha wanafunzi zaidi ya 250 kwa mwaka na kwa maana hiyo, wameweza
kuandaa vijana 250 kuingia kwenye vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi.
Akifafanua kuhusu malengo ya shule, Mkuu huyo wa shule alisema lengo lao ni
kutoa elimu bora kwa watoto wa Kitanzania na kuwandaa kuwa wawajibikaji kwa
Mungu na kwa Taifa lao.
Kwa upande wake, mwakilishi
wa wazazi wenye watoto waliohitimu kwenye mahafali hayo, bw. Eric Shigongo
alisema kila mhitimu anayo ndoto yake ambayo anapaswa kufanya kila awezalo
kuhakikisha ndoto yake inatimia.
“Unao uwezo wa kuchagua (power of
choice) kilicho chema kwa ajili ya maisha yako ya baadaye. Nasisitiza kwa
sababu najua kila mmoja wenu ana ndoto yake ya kufika mahali fulani. Hakikisha
unatimiza ndoto hiyo, haijalishi utapitia mazingira gani,” alisema.
Alisema kwake yeye anawaona vijana
waliohitimu kwamba ni washindi (champions) na aliwaeleza hivyo wiki tatu kabla
ya kuanza mitihani yao. Hata hivyo, aliwaasa kwamba wawe tayari kukosa mambo
mengine kama kweli wanataka kufanikiwa maishani mwao.
“kama unataka kufanikiwa maishani,
huna budi kujinyima mambo mengi ili uweze kupata kile unachokitaka. Najua
mmemaliza kidato cha sita lakini safari yenu ya maisha ndiyo kwanza imeanza.
Ninaamini wako watu hapa watakaotusaidia kutatua changamoto za nchi hii, wako
madaktari hapa, wako wahandisi, wako wafanyabiashara na yuko Rais ajaye wa Tanzania,
tena Rais mwanamke kutoka katika kundi hili,” alisema.
Katika mahafali hayo, mwanafunzi
Kauthar Said aliibuka mwanafunzi bora na kupewa zawadi ya kompyuta mpakato
(laptop) na wanafunzi wa mchepuo wa PCM, walipewa zawadi ya keki na Mkuu wa
Shule kwa kuwa ni darasa ambalo halijawahi kuwa na kesi yoyote ya utovu wa
nidhamu katika kipindi cha miaka miwili waliyoakaa shuleni hapo.
(mwisho)
IMETOLEWA:
JUMAPILI, MEI 14, 2017.
COMMENTS