Katika kuhakikisha Mkoa wa Rukwa Upo salama kutokana na maambukizi ya ugonjwa wa Ebola yatakayoweza kujitokeza, Mheshimiwa Mkuu wa Mk...
Katika
kuhakikisha Mkoa wa Rukwa Upo salama kutokana na maambukizi ya ugonjwa wa Ebola
yatakayoweza kujitokeza, Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Kamishna Mstaafu
Zelote Stephen amefanya ziara ya siku tatu katika mwambao wa ziwa Tanyangika
kwenye Kata ya Kirando, Kabwe na Kasanga vijiji ambavyo vipo jirani na nchi
ya DRC ili kujionea namna Halmashauri ya Nkasi na Kalambo zilivyojipanga
kuhakikisha kuwa ugonjwa huo hautii mguu katika Mkoa na nchi kwa ujumla.
Ziara hiyo aliianza siku ya Ijumaa
tarehe 26 hadi 28. 05. 2017 mara baada ya kumaliza kumalizika kwa mafunzo ya
siku tatu yaliyohusu utumaji wa taarifa za magonjwa kwa kieletroniki (e-idsr)
yenye kusisitiza tahadhari ya ugonjwa wa ebola uliopo katika nchi jirani ya
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) yaliyotolewa kwa wahudumu wa afya wa
Serikali na Sekta binafsi kwa Halmashauri mbili za Manispaa ya Sumbawanga na
Sumbawanga vijijini.
Mafunzo ya awamu ya pili yanatarajiwa
kumalizika tarehe 31. 05. 2017 kwa Halmashauri za Kalambo na Nkasi ikiwa ni
muendelezo wa awamu ya kwanza kwa Halmashauri ya Sumbawanga Vijijini na
Manispaa ya Sumbawanga yaliyoisha tarehe 26. Mwezi wa tano.
Ili kujiridhisha na maandalizi ya
Halmashauri zinazopakana na nchi za jirani yaani Jamhuri ya Kidemokrasia ya
Kongo (DRC) pamoja na Zambia Mkuu wa Mkoa alipita katika bandari maarufu za
pwani ya ziwa Tanganyika na kuongea na vyombo vya usalama ikiwemo uhamiaji,
Sumatra, TRA, jeshi la polisi, jeshi la wananchi, maafisa forodha pamoja na
maafisa afya kutoka Wilayani.
Pia Mh. Zelote aliongea na viongozi wa
serikali za vijiji na kata wakiwemo madiwani, watendaji wa kata na vijiji,
wenyeviti wa vijiji na vitongoji, maafisa ugani wa kata na vijiji, maafisa afya
wa kata na vijiji na kufanya mikutano ya hadhara ili kuwapa wananchi ujumbe
aliokwenda nao katika kuhakikisha ugonjwa huo haunusi katika mkoa wa Rukwa na
nchi ya Tanzania.
Pamoja nae Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa
aliambatana na Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Boniface Kasululu, Mratibu wa Chanjo
Mkoa Gwakisa Pamoja na Afisa kutoka Wizara ya Afya wa usimamizi na ufuatiliaji
Solomon Mushi, Mkuu wa Wilaya, makatibu tawala wa wilaya pamoja na kamati za
ulinzi na usalama za Wilaya.
Katika kila Wilaya aliyopita Mh. Zelote
alihakikisha anapewa taarifa za maandalizi ya Wilaya na kisha kwenda kwenye
mipaka ili kujionea kwa macho yake maandalizi hayo na pia kuongea na wananchi
wanoishi karibu na mipaka hiyo.
Wakati akiwa kwenye ziara hiyo Mh.
Zelote alikuwa akisisitiza utayari pamoja na kujihadhari kwa viongozi wa
serikali za vijiji na kata na pia kwa vyombo vya usalama vya maeneo hayo ya
mipakani.
Katika suala la utayari Mh. Zelote
Alisema kuwa wananchi wanapaswa kuelimishwa juu ya athari ya ugonjwa huo na
namna ya kujikinga nao ikiwa ni pamoja na kuelezwa dalili za ugonjwa na njia za
maambukizi ya ugonjwa huo na kuwasisitiza wananchi kwenda zahanati pindi
wanapojiskia kuumwa na sio kukimbilia kwenye maduka ya dawa na kuagiza vidonge
bila ya kujua ugonjwa anaoutibu.
Pia katika kusisitiza hilo Mh. Zelote
aliwasihi wananchi kutokimbilia kwa waganga wa kienyeji pindi wanapoumwa na
badala yake wakimbilie kwa wataalamu wa afya kwenye zahanati ama vituo vya
afya. Na kuwaonya kuwa kupitia hizi taarifa za ugonjwa wa ebola kunaweza
kukajitokeza matapeli ambao watajitangaza kuutibu ugonjwa huo jambo ambalo si
kweli, hivyo aliweka msisitizo kuwa ugonjwa wa Ebola hauna Tiba.
“Mtu yeyote atakayejiskia vibaya basi
haraka akimbilie kwenye zahanati ama kituo cha afya na sio kwa mganga wa
kienyeji, na mjiepushe mbali sana na matapeli wanaotibu watu vichochoroni
ama wanaosema dawa ya Ebola ipo,…. Hakuna,” Mh. Zelote alieleza.
Pamoja na hayo Mh. Zelote alionya kuwa
katika kusimamia jambo hilo hatakuwa na utani, dhihaka ama masihara kwayeyote
atakaekiuka taratibu zilizowekwa ili kujihadhari na ugonjwa huo kuingia katika
mkoa wa Rukwa.
“Mimi nafahamu kwamba watu wanaoishi
humu kwenye mipaka wameoa ama kuolewa katika nchi za jirani, na kwamba
watanzania utamaduni wetu ni ukarimu kwa wageni lakini katika hili tupunguze
ukarimu mpaka jambo hili liishe, na yeyote atakayegundulika anamhifadhi mgeni
kinyume na taratibu, huyo ni mhalifu,” Mkuu w Mkoa alisema.
Katika kuonesha athari kubwa inayoweza
kupatikana endapo uginjwa huo utapenya katika nchi yetu Mh. Zelote alieleza
kuwa gharama za kumshughulikia mgonjwa mmoja ni kubwa sana na kuongeza kuwa endapo
ugonjwa huo unathibitishwa kwenye nchi Fulani basi tatizo hilo si la nchi hiyo
tu ni la dunia nzima.
“Nguo inayotumika kumshughulikia mtu
mmoja inauzwa milioni 10 na kwa wenzetu huko afrika ya magharibi Ivory Coast
ambako walikumbana nao watu 11,000 walifariki, wakiwemo madaktari ambao
walikuwa wakiwauguza wagonjwa, mtu mmoja tu akiupata basi kijiji kizima
kinafungwa hakuna mtu kuingia katika kijiji hicho wala kutoka,” Mh. Zelote
alisisitiza.
Lakini pia aliwatoa hofu wananchi na
kuwaambia kuwa mpaka sasa Tanzania hakuna mgonjwa hata mmoja wa Ebola.
Nae Daktari wa Mkoa Dkt. Kasululu
alisema kuwa tangu ugonjwa huo kutolewa taarifa na Wizara ya Afya tarehe 12.
05. 2017 watu watatu wlikuwa wamefariki na wengine 12 walikuwa wako chini ya
uangalizi lakini hadi kufuikia tarehe 25. 05. 2017 idadi ya wagonjwa
iliongezeka hadi kufikia wagonjwa 45 na kuongeza kuwa idadi hiyo huenda
ikaongezeka kadiri siku zinavyokwenda mbele.
“Idadi ya wagonjwa imekuwa ikiongezeak
kila kukicha hivyo ni jukumu letu kuhakikisha tunajiandaa na kujihadhari kweli,
maana wagonjwa hawa wapo kwenye misitu ambapo usafiri wa kawaida haufiki
isipokuwa Helkopta na pikipiki, hivyo wagonjwa wanaweza kuwa wengi na bado
hawajajulikana,” Dkt Kasululu alisisiza.
Nae Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya ya
Nkasi Dk. Makundi Maige alielezea mikakakti ya Halmashauri ya Nkasi namna
ilivyojipaga kuhakikisha wanakaa mbali na ugonjwa hatari wa Ebola.
“ Wilaya imeainisha kata tatu za
Kirando, Kabwe na Wampembe ambazo zimetengwa kwaajili ya kupokea wageni kutoka
nchi za jirani, tukifahamu kuwa katika mwambao wa Ziwa Tanganyia kuna Kata 10
ambazo ugonjwa huu unaweza kuingia kwa urahisi, ambazo ni Kabwe, Kirando,
Wampembe, Itete, Kipili, Mkinga, Korongwe, Ninde, Kizumbi na Kala,” Dk. Makundi
aliainisha.
Katika kubainisha upokezi wa wageni hao
Dk. Makundi alisema kuwa kituo cha Wampembe kitapokea wageni wanoelekea kijiji
cha Kilambo hadi Msamba, Kituo cha Kirando kitapokea wageni wanaoelekea kijiji
cha Ninde hadi Kazovu na kituo cha Kabwe kitapokea wageni wanaoelekea kijiji
cha Utinta hadi Kalila.
Na kuongeza kuwa wageni wote kutoka
nchi za jirani watalazimika kupitia katika vituo hivyo na sio kuingia kiholela
kama ilivyozoeleka na kabla ya kuendelea na safari zao watakuwa wakichunguzwa
afya zao.
Kwa kuzingatia namna ugonjwa huo
unavyoenea Wilaya imetenga eneo maalum kwaajili ya matibabu ili kuepuka
kuchanganya wagonjwa watakaobainika kuwa na dalili za ugonjwa wa Ebola.
Pamoja na hayo Wilaya imejipaga
kuzizungukia kata zote 10 na kutoa elimu kwa wananchi na viongozi wa maeneo
hayo, ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha viongozi wa dini, wazee maarufu,
vijana, waalimu na wanafunzi juu ya ugonjwa huo hatari.
Nao upande wa Wilaya ya Kalambo
walieleza mipango yao juu ya udhubiti wa ugonjwa huu, ambapo mganga Mkuu wa
Wilaya Dkt. Alcado mwamba aliweza uainisha tahadhari mbalimbali ambazo Wilaya
imezichukua kuhakikisha wanaudhibiti ugonjwa huo kutokuingia katika Wilaya
hiyo.
Miongoni mwa tahadhari walizochukua
ikiwa ni kuwasambazia wananchi vipeperushi vyenye kutoa elimu ya ugonjwa wa
Ebola lakini pia kuihamasisha jamii kutoa taarifa haraka kwa uongozi wa
serikali pindi tu wakibaini kuna mgeni aliyeingia kinyume na taratibu
zilizowekwa.
COMMENTS