>>>Katavi wachimbaji, walinzi wapambana JESHI la Polisi mkoani Shinyanga limelazimika kupiga mabomu ya machozi na maji ya k...
>>>Katavi wachimbaji, walinzi wapambana
JESHI la Polisi mkoani Shinyanga limelazimika kupiga mabomu ya machozi na maji ya kuwasha kwa kundi la waendesha bodaboda zaidi ya 80.
Watu hao walikuwa wakiandamana katika eneo la Ibinzamata baada ya
mwenzao, Joel Mamla (26) kupoteza maisha juzi wakati alipokuwa anapelekwa Kituo cha Polisi mjini Shinyanga baada ya
kuvunja sheria za barabarani.
Jeshi hilo lililazimika kutumia kikosi cha Askari wa Kutuliza
Ghasia (FFU) kutuliza vurugu hizo, ambapo walitumia ‘section’ tano za askari,
ambapo kila ‘section’ yenye askari tisa ilitumika kuwatuliza waendesha bodaboda
hao baada ya kuwataka watawanyike kwa amani.
Kamanda wa Polisi
Mkoa wa Shinyanga, Jumanne Murilo, alithibitisha kutokea kwa vurugu. Alisema
waliamua kuzuia maandamano hayo kwa kutumia mabomu kwa sababu urushaji wa
mawe uliokuwa ukifanywa, ulionekana kuhatarisha hali ya usalama.
Alisisitiza kuwa maandamano hayo siyo si halali, na bodaboda
hawakupaswa kufanya hivyo, bali walitakiwa kutii sheria bila shuruti, na
kufuata taratibu za kudai kuonewa, na siyo kutishia kuharibu amani.
“Tulishaacha ule ukamataji wa bodaboda kwa kuwakimbiza, kwa sasa
anapovunja sheria tunamfuatilia taratibu na kumkamata kwenye mazingira ambayo
hayawezi kuhatarisha maisha yake,” alisema.
“Aliyefariki alifanya makosa na askari wetu wa usalama barabarani
Koplo Lwehendela alimfuatilia mpaka akamkamata na alikubali makosa na kukubali
kwenda kituo cha polisi. Baada ya kukubali, Lwehendela alimuelekeza Konstebo
Edmond ambaye ni askari wanaovaa kiraia afuatane naye hadi kituoni.
“Lakini alitumia ujanja na kumweleza askari kuwa pikipiki ina
matatizo hivyo askari apande ili waweze kuelekea kituoni, walipokuwa njiani
ndipo dereva huyo alipokuwa kwenye barabara inayoelekea Tabora- Tinde, ndipo
dereva huyo alipoongeza kasi ya pikipiki huku akiiyumbisha barabarani na
alikuwa akimwambia askari wetu kuwa lazima wafe wote.
“Aliendelea kwenda kwa kasi huku wananchi wakiwa wanashangaa nini
kilichotokea, ghafla waligonga nguzo pembeni ya barabara maeneo ya Huangija na
kuanguka kwenye shimo, ndipo alipofariki dereva na askari wetu kujeruhiwa
vibaya”, alisema.
Kamanda huyo alisema baada ya ajali hiyo juzi, jana walipata
taarifa kuwa kuna mwanasiasa (jina wamelihifadhi) ambaye anadaiwa kuwahamasisha
waendesha bodaboda takribani 1,000 kuandamana wakidai kuuawa. “Kuna mtu alikuwa
anashinikiza madereva wafanye maandamano, lakini wengi wa madereva hao
walionekana kutokubali na badala yake takribani 80 walifanya alivyokuwa
amewaambia.”
“Tulipambana nao na tuliweza kurudisha amani. Na kwenye mchakato
huo walipasua kioo cha mbele cha gari letu lenye namba PT 3705 kwa mawe
waliyokuwa wakirusha. Lakini jeshi letu liliweza kuwakamata 28 na pia
walikamata pikipiki 86 baada ya waandamanaji kukimbia na kuziacha,” alisema
Murilo.
Taarifa za awali za tukio hilo, zinaeleza kuwa jeshi hilo
lilitumia takribani saa sita ili kuwatawanya waendesha bodaboda hao,
waliokuwa wakiandamana huku wakirusha mawe, kupinga kitendo cha mwenzao
kufa wakidai kifo hicho kimesababishwa na askari polisi.
Hata hivyo,
mshangao uliibuka kwa wananchi wa manispaa ya Shinyanga baada ya baadhi ya
askari wa kikosi cha kutuliza ghasia, kuwatawanya waombolezaji waliokuwa
katika msiba wa Mamla, kwenye nyumba aliyokuwa akiishi dereva huyo jana na
kuzua taharuki zaidi.
Baadhi ya
waendesha bodaboda, Simoni Bundala na Ramadhani Faraji walisema
wameamua kuandama kwa madai ya kutaka kufikisha ujumbe ili serikali
ione Polisi mkoani Shinyanga isivyotenda haki, bali linawaonea.
Faraji alisema haiwezekani askari aliyevaa kiraia akamate pikipiki yenye makosa bila hata ya kuonesha kitambulisho, jambo ambalo ni hatari kwa kuhofia unyang'anyi wa pikipiki.
“Tukio la juzi bodaboda mwenzetu Joel (Mamla) mkazi wa mjini humo alikufa katika ajali iliyosababishwa na askari aliyemkamata kumkaba shingo hadi kusababisha ajali wakati akimlazimisha kwenda kituo cha polisi," alisema Bundala.
Huko Mpanda, vurugu zimeibuka katika machimbo ya
madini ya dhahabu ya Isumamilo wilayani
Mpanda katika mkoa wa Katavi baina ya
wachimbaji wadogo wapatao 6,000 na walinzi wa machimbo na kusababisha kibanda
cha kupimia madini hayo na ofisi
kuchomwa na kuteketea kwa moto.
Kufuatia vurugu hizo, walinzi wa machimbo hayo
walilazimika kufyatua risasi za moto hewani
ili kuwatawanya wachimbaji hao wadogo.
Kaimu Kamanda
wa Polisi wa Mkoa wa Katavi, Benedict Mapujila amethibitika kutokea kwa tafrani
hiyo na alisema vurugu hizo zilidumu zaidi ya saa moja zilitokea jana
saa 2:30 asubuhi.
Alisema kuwa
hadi sasa hakuna mtuhumiwa yeyote aliyekamatwa
wala hakuna mtu yeyote
aliyepoteza maisha na Polisi inaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.
Mapujila
alisema vurugu hizo zilisababishwa na
walinzi wa machimbo hayo, kumkamata mchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu akiwa
na madini hayo akitaka kutoroka.
“Baada ya
mchimbaji huyo mdogo wa madiniya dhahabu
kukamatwa na walinzi hao kumshambulia kwa kumpiga mateke na marungu kitendo ambacho
kiliwakasilisha wachimbaji wenzake
wakilalamika kuwa imekuwa ni tabia ya
walinzi wa machimbo hayo kuwapiga wachimbaji," alieleza Mapujila.
Akisimulia
mkasa huo, alisema kuwa kundi kubwa la wachimbaji hao wadogo wakiwa na hasira,
walijikusanya na kuanza kuvamia kibanda cha walinzi na ofisi ya kupimia madini
hayo na kuteketeza kwa moto.
“Wakati
wachimbaji hao wakiteketeza kibanda
hicho kwa moto walinzi wa machimbo hayo walilazimika
kufyatua risasi za moto hewani
lakini wachimbaji hao hawakujali
waliendelea bila kujali risasi,” alieleza Kaimu Kamanda huyo.
Mkuu wa
Mkoa wa Katavi, Raphael Muhuga alifika
kwenye eneo hilo na kusikiliza kero mbalimbali zilizotolewa na wachimbaji hao
wadogo na aliwataka wafuate
taratibu zilizowekwa na Serikali
kulalamika.
“Kiitendo
cha wachimbaji kutorosha dhahabu
bila kupima kunasababisha Serikali kukosa mapato
yatokanayo na madini hayo," aliwaeleza.
Machimbo
ya Isumamilo yamekuwa
maarufu kwa kipindi cha miezi
minne sasa kutokana na kugundulika kwa
dhahabu nyingi. Wachimbaji wadogo 6,000
kutoka mikoa mbalimbali nchini hususani ya Kanda ya Ziwa, huchimba
madini hapo.
Source:HabariLeo
Source:HabariLeo
COMMENTS