Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) inaungana na wadau wote wa haki za watoto duniani katika kuadhimisha “Siku y...
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora (THBUB) inaungana na wadau wote wa haki za watoto duniani katika
kuadhimisha “Siku ya mtoto wa Afrika”.
Siku hii inaikumbusha dunia juu ya mauaji ya watoto wapatao 2,000 wa kitongoji
cha Soweto nchini Afrika Kusini, waliouawa kikatili miaka 41 iliyopita na
iliyokuwa Serikali ya Makaburu.
Siku hii ilizinduliwa rasmi mwaka
1991 na uliokuwa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU) ili kuwakumbuka watoto hao
waliokuwa wakidai haki ya kutobaguliwa na haki nyingine za binadamu.
Wakati tunaadhimisha siku hii
muhimu wadau wote wa haki za watoto hatuna budi kujitathimini namna tunavyowaandaa
watoto wetu ili waweze kutoa mchango stahiki katika maendeleo ya taifa letu,
kwa kuzingatia kauli mbiu ya mwaka huu inayosema: “Maendeleo endelevu 2030: Imarisha ulinzi na fursa kwa watoto wote.”
Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizochukua hatua
mbalimbali kuhakikisha uwepo wa maslahi ya watoto. Hatua hizo ni pamoja na kutunga
sheria na kuridhia mikataba mbalimbali ya kimataifa na kikanda inayolinda na
kutetea haki za mtoto. Mikataba hiyo inajumuisha: Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Mtoto (1989), Tamko la Shirika la Kazi
Duniani (ILO) Na. 182, na Mkataba wa Afrika wa Haki na Ustawi wa Mtoto (2003).
Miongoni mwa sheria zilizotungwa katika
ngazi ya kitaifa ni: Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977), Sheria
ya Mtoto Na. 21/2009, Sheria ya Kanuni za Adhabu, Sheria
ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai na Sheria ya Makosa ya Kujamiiana – SOSPA
(1998).
Pia
imeridhia na kubuni sera, mipango na mikakati mbalimbali ya kitaifa na
kimataifa, ikiwemo: Sera ya Mtoto
(2008), na Mpango-kazi wa Kitaifa wa Kuzuia na Kupambana na Ukatili dhidi ya
Wanawake na Watoto (2017- 2022).
Kimataifa imeridhia na inatekeleza Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu ya Dunia (SDG’s)
yaliyopitishwa mwaka 2015 yanayobainisha kuwa watoto wana haki
ya kuishi, kulindwa, kutobaguliwa na kushirikishwa kwa usawa ili kuhakikisha kuwa wanapata fursa sawa
katika jamii.
Ili kuhakikisha kuwa Tanzania
inakuwa kinara wa kujali haki za watoto Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania pia imeanzisha taasisi na vyombo mbalimbali vinavyoshughulikia ulinzi
na ukuzaji wa haki za watoto nchini. Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
ni miongoni mwa taasisi hizo.
Tume imekuwa ikitoa elimu ya haki
za binadamu, ikiwemo haki za watoto kupitia vyombo vya habari, semina na
mikutano mashuleni na maeneo mbalimbali
inayopata fursa ya kuyafikia.
Pia, Tume imekuwa ikitoa huduma za
kisheria kwa makundi yenye uhitaji ambao ni pamoja na watoto na watu wengine
wenye uhitaji wa msaada wa kisheria na pia imeanzisha dawati mahsusi
linaloshughulikia haki za watoto.
Vilevile, Tume imekuwa
ikishirikiana na wadau mbalimbali wa haki za binadamu kimataifa na kitaifa ili
kuweka nguvu ya pamoja katika kulinda haki za binadamu na kukemea vitendo vya
ukatili na unyanyasaji dhidi yao.
Aidha, kupitia Mpango-kazi wa
Kitaifa wa Haki za Binadamu (National Human Rights Action Plan - 2013-2017)
Tume imefanikiwa kutoa mafunzo kwa waalimu na watendaji wengine katika sekta ya
elimu na kuhamasisha uanzishwaji wa vilabu takriban 130 vya haki za binadamu shuleni. Pamoja na mambo mengine vilabu
hivi vinajihusisha na utoaji wa elimu ya haki za binadamu ikiwemo elimu ya haki
za watoto, shuleni na nje ya shule.
Juhudi hizo ni muhimu kipindi hiki
katika kuunga mkono dhamira ya Serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. John Pombe Magufuli katika kuhakikisha kuwa
Tanzania inafikia azma yake ya “Kujenga
Tanzania ya Viwanda.”
Pamoja na jitihada hizi zote bado zipo
changamoto mbalimbali zinazoathiri malezi ya watoto na kuwanyima fursa katika
jamii, changamoto hizo ni pamoja na: umaskini, migogoro ya wanandoa, mila
potofu, utandawazi, majukumu ya kijinsia katika jamii na ukosefu wa haki ya
elimu ya afya ya uzazi (reproductive and health rights).
Tume inaitaka jamii kuwapa umuhimu
watoto wa kike na kuachana na mtazamo potofu kuwa hawana mchango mkubwa kwa
jamii, hali inayochangia utumikishwaji wa watoto na kujiingiza katika mahusiano
ya kimapenzi na biashara ya ngono katika umri mdogo.
Vitendo hivyo vimekuwa chanzo cha
mimba na ndoa za utotoni ambazo huwaletea madhara mbalimbali ikiwemo:
unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia, kingono, athari za kiafya, vifo wakati wa
ujauzito/kujifungua na maambukizi ya Virusi vya UKIMWI (VVU).
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na
Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia idadi ya watu Duniani (UNFPA)
mwaka 2014, tatizo la ndoa za utotoni lipo duniani kote. Takriban wasichana
milioni 15 wanaolewa kila mwaka chini ya umri wa miaka 18. Ikiwa ni wastani wa
watoto wa kike 41,000 kwa siku.
Utafiti huo ulibaini kuwa tatizo la
mimba za utotoni kwa Tanzania ni kubwa, ambapo wasichana 4 kati ya 10 (sawa na
asilimia 40) wanaolewa kabla ya kufikisha umri wa miaka 18.
Pia kwa mujibu wa takwimu za
demografia ya afya Tanzania (TDHS, 2016) asilimia 36 ya wanawake wa kitanzania
wenye umri wa miaka kati ya 20-24 waliolewa au waliingia kwenye mahusiano ya
kimapenzi kwa mara ya kwanza kabla ya kutimiza umri wa miaka 18.
Takwimu zilizotolewa na Shirika la
Watoto Duniani (UNICEF, 2012) zimeitaja Mikoa inayoongoza kwa ndoa za utotoni kuwa
ni: Mkoa wa Shinyanga ukiongoza kwa asilimia 59. Ikifuatiwa na Tabora (58%),
Mara (55%), Dodoma (51%) na Lindi (48%).
Hivyo basi, Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora inapendekeza na kutoa wito kama ifuatavyo:
1. Serikali ifanye marekebisho ya sheria kandamizi na zinazopingana
na sheria zingine. Mfano;- Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 inaweka miaka 18 kuwa
umri mdogo ambao wavulana wanaruhusiwa kuoa, lakini imeweka umri wa miaka 15
kwa wasichana kuolewa kwa ridhaa ya wazazi.
2. Mamlaka zinazotoa haki kwa wahanga wa ukatili,
wakiwemo watoto zitoe haki kwa wakati.
3. Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya
Ufundi ihakikishe uwepo wa mfumo utakaowawezesha watoto wa kike wanaopata mimba
mashuleni kuendelea na masomo yao mara tu wanapojifungua.
4. Wadau wa haki za binadamu waendelee kutoa elimu ya
haki za binadamu kwa jamii, ili kubadili mila na tamaduni potofu. Pia kukemea
vitendo vya ukatili, unyanyasaji na udhalilishaji wa watoto.
5. Wazazi wawajibike katika malezi ya watoto ili
kuimarisha familia zao na kuwaepusha na viashiria hatarishi kwa maisha ya
watoto wao.
6. Watoto wapatiwe elimu ya afya ya uzazi ili waweze
kujitambua na kuwa na uelewa juu ya madhara ya mimba na ndoa za utotoni.
7. Wadau mbalimbali wa haki za watoto kuhakikisha kuwa
ulinzi, usalama na haki za mtoto vinaimarishwa. Aidha, wahakikishe watoto wa
kike na wa kiume wanapatiwa malezi bora yanayotoa fursa sawa kwa wote ili
kuhakikisha kuwa ndoto zao katika maisha zinafikiwa.
8. Wadau wote wa haki za binadamu kuhakikisha kuwa
kama taifa tunaondoa aina zote za ukatili na ubaguzi dhidi ya watoto na kuwapa
haki na fursa sawa katika umiliki wa rasilimali na nyanja zote za kimaisha na
kusimamia Sheria na Sera zinazolinda usawa wa kijinsia ili taifa letu liweze
kufanikisha lengo la fursa sawa kwa wote ifikapo mwaka 2030.
Imetolewa na:
(SIGNED)
Salma Ali Hassan
(Kamishna)
TUME YA HAKI ZA
BINADAMU NA UTAWALA BORA
Juni 16, 2017
COMMENTS