Balozi wa China nchini, Mh. Wang Ke (wa tatu kulia) akisalimiana na mwakilishi wa mgeni rasmi Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uwekezaji w...
Balozi wa China nchini, Mh. Wang Ke (wa tatu kulia)
akisalimiana na mwakilishi wa mgeni rasmi Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya
Uwekezaji wa Wizara ya Viwanda, Biashara
na Uwekezaji, Aristide Mbwasi (kulia) mara baada ya kuwasili ukumbini wakati wa
hafla maalumu ya chakula cha jioni kwa wateja wa benki hiyo wa makampuni ya
China nchini Tanzania iliyofanyika katika hoteli ya Serena jijini Dar es
Salaam. Wengine katika picha ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard
Chartered nchini, Sanjay Rughani (wa pili kulia), Mjumbe wa Bodi ya Standard
Chartered nchini, Ami Mpungwe (wa pili kushoto) na Mkuu wa Mahusiano na Masoko
wa Benki ya Standard Chartered, Juanita Mramba (kushoto).
CHINA katika kipindi cha miaka mitatu ijayo inatarajia
kuwekeza katika viwanda 200 nchini Tanzania vitakavyokuwa na uwezo wa kuajiri
moja kwa moja Watanzania laki mbili.
Kwa sasa uwekezaji wa China nchini Tanzania umetoa fursa za
ajira za moja kwa moja 150,000 na
zisizokuwa za moja kwa moja 350,000.
Taarifa hiyo imetolewa na Waziri wa Viwanda, Biashara na
Uwekezaji, Mh. Charles Mwijage katika hafla
ya chakula cha jioni kwa wawekezaji kutoka China iliyoandaliwa na Benki
ya Standard Chartered.
Aidha Waziri Mwijage alisema amefurahishwa na kauli
iliyotolewa na Benki hiyo kwamba inawekeza dola za marekani bilioni 20 sawa na
fedha za kitanzania trilioni 40 katika kampeni ya China ya uwezeshaji mitaji na
biashara kutoka Asia kwenda nchi nyingine za dunia.
Kampeni hiyo inayoitwa One Belt One Road inagusa nchi 65,
Tanzania ikiwamo.
Aliisifu Benki hiyo kwa kuandaa hafla hiyo kwa wateja wake wa
China ikiwa ni sehemu moja ya kutangaza kampeni
hiyo ya China na kuwafanya wananchi wengi kuelewa fursa zinazoambatana
nazo.
Alisema kwa sasa Tanzania inapigana kuingia katika uchumi wa
kati unaoendeshwa na viwanda na kampeni ya China inakwenda sawa na mpango wa
maendeleo wa miaka mitano uliokazania uwekezaji katika viwanda.
Alisema kwa sasa Serikali inaweka vyema mazingira ya uwekezaji
na ikiwa na uchumi unaokua kwa kasi wa asilimia
6 hadi 7 juhudi za Benki hiyo za kuonesha fursa za uwekezaji na
uendeshaji wa uchumi zinakaribishwa na
serikali ya Tanzania.
Aidha katika hotuba hiyo iliyosomwa na Kaimu Mkurugenzi wa
Idara ya Uwekezaji wa Wizara ya Viwanda,
Biashara na Uwekezaji, Aristide Mbwasi alisema kwamba mpango huo wa China
unaozungumzia uwezeshaji wa mitaji na biashara kutoka Asia kwenda nchi nyingine
ni kichocheo cha kukua kwa chumi mbalimbali duniani na kutaka watanzania kushiriki
kikamilifu.
Awali Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo nchini Tanzania,
Sanjay Rughani alisema kwamba Benki ya
Standard Chartered duniani inawekeza katika Belt and road Initiative kiasi cha
dola bilioni 20 sawa na shilingi trilioni
44.8 za Kitanzania kuwezesha miradi mbalimbali kwenye kampeni hiyo ya China.
Alisema mwaka jana pekee benki hiyo iliingiliana mikataba
katika miradi 40 kwenye nchi mbalimbali za mradi huo.
“Standard Chartered imewekeza katika nchi 45 za kampeni ya belt
and Road zenye msukumo mkubwa wa shughuli zikiwemo nchi za Kusini Mashariki mwa
Asia, Kusini mwa Asia na Afrika” alisema na kuongeza kuwa kazi yao kubwa ni
kutoa mitaji ya kifedha ikiwamo mikopo na kuwezesha miamala mbalimbali.
Aidha alisema asilimia 50 ya mikataba hiyo na shughuli
zilizofanywa kwa mwaka 2017 zilikuwa Afrika huku asilimia 25 zikienda Kusini
mwa Asia na nyingine ni katika maeneo mbalimbali ya kampeni.
Alisema pamoja na kuishiriki moja kwa moja pia benki ya
Standard imekuwa ikishirikiana na taasisi nyingine za fedha kusaidia wateja
mbalimbali wa kwenye kampeni hiyo.
Alitaja washirika wao wengine kuwa AIIB, Silk Road Fund, China
Development Bank, China Exim Bank na benki nyingine za kibiashara za China.
Alisema ikiwa na historia ya miaka 150 na kuaminika vya
kutosha na wateja mbalimbali wamekuwa wakitumia utaalamu na elimu waliyonayo
katika kutengeneza mazingira bora ya uwekezaji katika nchi zinazohusika na
kampeni ya mitaji kutoka asdia kwenda nchi nyingine.
Rughani alisema
benki hiyo ina madawati katika
nchi mbalimbali yanayoshughulikia wawekezaji kutoka China kwa lengo la
kuwawezesha kutambua mazingira ya uwekezaji katika nchi husika na kuwafanya
wawe na uhakika na uwekezaji wao.
Katika hafla hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na Balozi wa China
nchini Tanzania, Wang Ke alisema kwamba taifa lake linaendelea kutoa
ushirikiano mkubwa kuwezesha maendeleo kwa nchi washirika katika kampeni
iliyoanzishwa takribani mikaa mitatu iliyopita ambayo inakwenda hadi mwaka
2020.
Alisema amefurahishwa sana na juhudi za Benki hiyo katika
kutumia fursa iliyonayo kuhamasisha uwekezaji na kuwezesha China na washirika
wake wa maendeleo kuwa na uhakika na shughuli na fursa za uwekezaji kwa
kuzingatia kampeni ya One Belt One Road.
Biashara ya China na mataifa hayo 65 katika kampeni hiyo,
ilizidi dola za Marekani trilioni 3 kati ya mwaka 2014 hadi 2016 na kwamba
uwekezaji wa moja kwa moja wa China katika nchi hizo umepita dola za Kimarekani
bilioni 129 kufikia mwaka 2016 kutoka dola bilioni 92 mwishoni mwa mwaka 2014.
COMMENTS