Na Mwandishi wetu Kiwango cha shehena kilichohudumiwa na Bandari ya Tanga baada ya maboresho kimekuwa kikiongezeka kwa wastani wa asilim...
Na Mwandishi wetu
Kiwango cha shehena kilichohudumiwa na Bandari ya Tanga baada ya maboresho kimekuwa kikiongezeka kwa wastani wa asilimia 12.2 kwa mwaka.
Shehena iliongezeka kutoka tani za mapato 667,976 mwaka 2018/19 hadi tani za mapato 987,828 mwaka 2022/23, alisema Meneja wa bandari hiyo Masoud Mrisha akizungumza na wahahariri wandamizi wa vyombo vya habari mwishoni mwa wiki.
Aidha alisema ya meli za kimataifa na mwambao zilizohudumiwa zimeongezeka kutoka meli 125 Mwaka 2018/19 hadi meli 197 Mwaka 2022/23 sawa na wastani wa ongezeko la asilimia 16.2 kwa mwaka.
Pia ukubwa wa meli (GRT) umeongezeka kutoka GRT 677,922 mwaka 2018/19 hadi GRT 969,986 mwaka 2022/23 sawa na ongezeko la 11.3%.
Idadi ya jumla ya makasha yaliyohudumiwa iliongezeka kutoka Makasha 6,259 TEUs kwa mwaka 2018/19 hadi Makasha 7,244 TEUs kwa mwaka 2022/23, sawa na ongezeko la wastani wa asilimia 4.3 kwa mwaka.
Pamoja na maboresho katika Bandari ya Tanga bado Bandari ya Tanga ina changamoto ya upatikanaji wa shehena ya makasha sababu kubwa ikiwa ni uhaba wa shehena ya kupeleka nje ya nchi (Export), hii inapelekea wamiliki wa meli kutoleta meli kubwa na hivyo Bandari ya Tanga kuhudumia feeder vessels kwa shehena ya makasha.
Akifafanua zaidi manufaa ya maboresho hayo Masoud alisema shehena iliyohudumiwa katika kipindi cha Julai 2023 – Machi 2024, kwa mwaka wa fedha 2023/2024 ilifikia tani 868,957 DWT ikiwa ni sawa na asilimia 116.1 ya shehena iliyohudumiwa kawa kipindi kama hicho kwa mwaka wa fedha 2022/23 ambapo jumla ya tani 748,742 DWT zilihudumiwa.
Jumla ya meli 217 zenye ukubwa wa GRT 1,160,799 zilihudumiwa katika kipindi cha Julai 2023 hadi Febuari, 2024.
Aidha akitoa mchanganuo alisema meli 94 zilikuwa za Kimataifa (Deep Sea) na Meli 123 zikiwa meli za Mwambao (Coastal vessel). Idadi hiyo ya meli zilizohudumiwa ni asilimia 35.6 juu ya meli zilizohudumiwa kipindi kama hicho kwa mwaka 2022/23 ambapo meli 160 zenye ukubwa wa GRT 710,655 zilihudumiwa.
Mafanikio hayo yametokana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Uchukuzi chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) kutekeleza miradi miwili ya kimkakati katika awamu mbili yenye jumla ya thamani ya fedha Sh 429.1.
Katika awamu ya kwanza Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania iliingia mkataba na Mkandarasi M/S China Habour Engineering Company (CHEC) Agosti 3,2019 na kuanza rasmi utekelezaji wa kazi mwezi Oktoba 2019 na kukamilika mwezi Juni 2022 kwa thamani ya Sh bilioni 172.3.
Pia mnamo Oktoba 24, 2019 TPA iliingia mkataba na kampuni za M/s NIRAS A/S (AS A LEAD Firm) ya Denmark kwa ushirikiano na M/S Maritime & Transport Business Solution, M/S ILF Consulting Engineers na M/S Anova Consult Company Limited ya Tanzania kwa kufanya upembuzi yakinifu na kusimamia mikataba ya ujenzi wa gati pamoja na kuongeza kina (draft) katika Bandari ya Tanga kwa niaba ya TPA.
Mradi huu ulihusisha upanuzi wa eneo la kuingia na kutoka Bandarini (entrance channel) lenye upana wa mita 73, kuongeza kina cha maji (dredging) kutoka mita 3 hadi kufikia mita 13 (draft),upanuzi wa eneo la kugeuzia meli (turning basin) kuwa na kipenyo cha mita 800 na ununuzi wa mitambo kumi na sita (16) ya kuhudumia shehena.
Aidha katika awamu ya pili Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania iliingia mkataba na Mkandari M/S China Habour Engineering Company (CHEC) Julai 30, 2020 kwa ajili ya kuboresha Bandari ya Tanga awamu ya pili na kuanza kazi mnamo tarehe 16 Disemba 2020.
Mradi huo ulihusisha ujenzi wa gati lenye urefu wa mita 450, kina cha mita 13CD na yadi ya makasha (Container yard) ya mita za mraba 7,230. Gati hili lina uwezo wa kuhudumia meli za makasha 2 zenye urefu wa mita 220 na kubeba tani mpaka 60,000 kwa wakati mmoja.
Bandari ya Tanga ni miongoni mwa Bandari kuu tatu za mwambao wa Bahari ya Hindi, zilizo chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA).
Bandari ya Tanga ilianzishwa miaka ya 1880 na Ukoloni wa Kijerumani ikijulikana kama “Marine Jetty”. Ujenzi wa gati ya kwanza lenye urefu wa mita 221 ulifanyika mwaka 1914, na gati ya pili lenye urefu wa mita 229 mnamo mwaka 1954. Gati zote mbili zenye jumla ya urefu wa mita 450 zilikuwa na kina cha maji (draft) mita 3 na uwezo wa kuhudumia shehena tani 750,000 kwa mwaka. Hali hiyo ilisababisha Bandari kutokuwa na uwezo wa kupokea meli gatini, na kufanya kazi ya upakuaji na upakiaji kufanyika nangani umbali wa Kilometa 1.7 kutoka gatini.
Aidha, eneo la Bandari ya Tanga lina jumla ya Hekta 400 ambapo Hekta 17 kati ya hizo ndipo ilipo Bandari ya sasa, Hekta 176 zipo eneo la Mwambani na Hekta 207 zipo katika kijiji cha Chongoleani eneo ambalo linatarajiwa kujengwa gati ya kuhudumia shehena ya Mafuta.
COMMENTS